WAZIRI WA KILIMO AWATAKA WATUMISHI WA WIZARA YA KILIMO KUISOMA ILANI YA UCHAGUZI YA CCM ILI KUJIANDAA NA UTEKELEZAJI WAKE

Na Mathias Canal, Wizara ya Kilimo-Dodoma
Watumishi wa Wizara ya Kilimo wameagizwa kuisoma ilani ya Chama Cha Mapinduzi iliyotolewa na Halmashauri kuu ya Taifa ya CCM Agosti 2020 kwa ajili ya uchaguzi Mkuu wa Mwaka huu.


Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga ametoa agizo hilo wakati akizungumza kwenye kikao cha dharula na Menejimenti na watendaji wakuu wa Bodi za mazao pamoja na Taasisi zilizo chini ya Wizara ya Kilimo kilichofanyika Jijini Dodoma Leo tarehe 31 Agosti 2020.

Waziri Hasunga amesema kuwa Ilani ya CCM ina mambo mengi makubwa na muhimu ya kuhusu sekta ya kilimo ambayo yameainishwa katika ukurasa wa 33 mpaka ukurasa wa 46.

Maeneo hayo ambayo CCM imebainisha ili serikali yake itakapopewa dhamana kwa mara nyingine iyatekeleze ni pamoja na usimamizi madhubuti wa Programu ya kuendeleza sekta ya kilimo Awwamu ya Pili (ASDP II) kwa kusimamia kwa weledi matumizi bora ya ardhi pamoja na maji ili kuwa na kilimo chenye tija.

Kuongeza uzalishaji wa mbegu bora za kilimo, Usimaizi madhubuti wa mbolea na viuatilifu ili kuondokana na changamoto ya viuatilifu na mbolea feki kadhalika kuhusu umuhimu wa kuongeza maeneo ya umwagiliaji ikiwa ni pamoja na usimamizi madhubuti wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji nchini ili kuondokana na dhana ya kutegemea kilimo cha msimu badala yake kuhamia katika kilimo cha Umwagiliaji, Tija na kuongeza uzalishaji.

Katika kikao hicho kilichohudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Ndg Gerald Kusaya na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo Prof Siza Tumbo, Waziri Hasunga amemuagiza kila mtumishi wa serikali katika Wizara ya Kilimo kuitafuta na kuisoma ilani ya uchaguzi ili kutafakari na kujiandaa kwa ajili ya utekelezaji wake kwani imani yake CCM itashinda kwa kishindo na hivyo kuendelea kuongoza dola.

Amesema kuwa katika ukurasa wa juu wa ilani uliopambwa na kauli mbiu isemayo “Tumetekeleza kwa Kishindo, Tunasonga mbele Pamoja” ilani inaonyesha dira na muelekeo wa utendaji wa shughuli mbalimbali za wizara ya kilimo ambapo miongoni mwa picha kumi zilizowekwa juu ni picha mbili zinahusu sekta ya kilimo hivyo ilani ya CCM imeonyesha umuhimu wa sekta ya kilimo nchini.

Ilani hiyo yenye kurasa 303 katika ukurasa wa 30 mpaka 33 imebainisha umuhimu wa usimamizi wa sekta ya Ushirika ikiwemo kusimamia masoko ya wakulima kadhalika kuongeza tija ya usiamamizi wa vyama vya Ushirika nchini ili kuwanufaisha wakulima nchini.

MWISHO


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527