TUTUMIE FURSA ZA NANENANE KUPATA ELIMU

strong>
Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) Xavery Mkingule (katikati kulia) akielezea maendeleo ya kazi za Shirika kwa Mrajis wa Vyama vya Ushirika Dkt. Benson Ndiege wakati wa Maonesho ya Nanenane Mkoani Simiyu

Mrajis wa Vyama vya Ushirika na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Dkt. Benson Ndiege akiangalia bidhaa ya Mafuta ya mawese kutoka Chama cha Ushirika cha Msingi Umoja Amcos Kyela Mbeya,kushoto ni Meneja wa Chama hicho Mboka Mwaijande wakati wa Maonesho ya Nanenane Viwanja vya Nyakabindi Mkoani Simiyu
Mrajis Dkt. Ndiege akieleza jambo kwa Mwenyekiti wa Chama Kikuu cha Ushirika TANECU Shaibu Sadiki wakati wa maadhimisho ya Nanenane, Mkoani Simiyu

...........................................................................................

Mrajis wa Vyama vya Ushirika na Mtendaji Mkuu wa Tume ya Maendeleo ya Ushirika Dkt. Benson Ndiege ametoa wito kwa wakulima, wanaushirika na wadau wengine kushiriki katika maonesho ya Sikukuu ya Wakulima Nanenane 2020, yanayoendelea nchini kwa lengo la kupata elimu ya masuala mbalimbali hususani Ushirika.

Mrajis ameyasema hayo Agosti 02, 2020 wakati wa maonesho ya Sikukuu ya Wakulima Kitaifa yanayoendelea Kitaifa Viwanja vya Nyakabindi Mkoani Simiyu. Maonesho ambayo mwaka huu yana Kauli mbiu isemayo “kwa maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi Chagua Viongozi Bora 2020”

Dkt. Ndiege amefafanua kuwa Tume ya Maendeleo ya Ushirika imeshiriki Nanenane Jijini Dodoma pamoja maonesho ya Kitaifa Mkoani Simiyu na kuongeza kuwa mwaka huu Tume imeshiriki kipekee katika mfumo wa “Kijiji cha Ushirika”.

Jambo ambalo alilieleza kuwa ni mkusanyiko wa wadau mbalimbali wa Ushirika pamoja na Tume ya Maendeleo ya Ushirika katika eneo moja la Viwanja vya Nyakabindi kwenye maonesho ya Nanenane. Akitaja baadhi ya wadau walioshiriki katika kijiji hicho ni pamoja na Vyama vya Ushirika wa mazao, vyama vya Ushirika wa Akiba na Mikopo, Mashirika yasiyo ya Kiserikali, Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO), Chuo cha Ushirika Moshi (MoCU) na taasisi nyingine za Ushirika.

“Tume inawakaribisha wadau mbalimbali kuendelea kufika katika maonesho ya Nanenane kujifunza masuala ya Ushirika ikiwemo masuala ya utunzaji wa taarifa za ushirika, misingi ya Ushirika, Sheria za Vyama vya Ushirika pamoja na kubadilishana uzoefu wa masuala mbalimbali ya kiushirika,” alisema Dkt. Ndiege

Ushirika ni miongoni mwa Taasisi ambazo zinaisadia sana Serikali katika kutoa ajira kwa vijana, wanawake na wananchi wengine na hivyo kupunguza changamoto ya ajira katika nchi yetu. Aidha, ajira zinazotolewa katika Vyama vya Ushirika ni zenye staha na kuleta heshima kwa jamii kwani hutoa ajira za uhakika na hakuna utaratibu wa kuwafukuza wafanyakazi ovyo bila kufuata sheria, kanuni na taratibu za Ushirika.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Ukaguzi na Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (COASCO) Xavery Mkingule wakati wa maonesho hayo akieleza hali ya ukaguzi wa Vyama vya Ushirika kwa mwaka 2019/20 alifafanua kuwa malengo yaliyopangwa na Serikali kwa COASCO ni kukagua Vyama hai vya Ushirika 6,463. Akifafanua kuwa utekelezaji umefanyika ukaguzi wa vyama 6,006 vimekaguliwa hadi kufikia tarehe 30.06.2020.

Mkurugenzi Mkingule aliongeza kuwa baadhi ya Vyama vya Ushirika vimekuwa vikipata hati zisizoridhisha kutokana na kutokuwa na uelewa mzuri wa uandishi sahihi wa kumbukumbu za taarifa za miamala ya shughuli zinazofanyika kwenye Vyama vya Ushirika.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527