MGANGA MKUU WA SERIKALI AWAAGIZA WAGANGA WAKUU WA MIKOA NA WILAYA KUONGEZA JITIHADA KATIKA KUPUNGUZA VIFO VYA MAMA NA MTOTO

NA WAMJW- KILIMANJARO

MGANGA Mkuu wa Serikali Prof. Abel Makubi ameagiza ndani ya miezi sita (6) Waganga Wakuu wote wa mikoa, Waganga Wakuu wa Wilaya na Waganga wafawidhi wa hospitali zote nchini kuongeza kasi katika kupunguza zaidi vifo vya mama na mtoto kwa kuboresha huduma na usimamizi katika maeneo yao.


Mganga Mkuu wa Serikali ametoa agizo hilo jana wakati wakati akiongea na Watumishi wa hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mawenzi-Kilimanjaro kwenye ziara yake ya kukagua hali ya utoaji huduma na ujenzi wa miundombinu ya afya katika Mkoa huo.

“Waganga Wakuu wote wa Mikoa, Wilaya pamoja na Waganga wafawidhi wa Hospitali zote mlifanyie kazi hili suala la kupunguza zaidi vifo vya akina mama wajawazito, nawapa miezi mitatu hadi sita, nione hali ya vifo vinakushuka zaidi kila mkoa, na Wilaya, na pamoja na Waganga wafawidhi wa Hospitali zote za kanda na Wilaya, itakavyofika miezi sita nitafanya ufuatiliaji kwa kushirikiana na TAMISEMI, Kiongozi ataeshindwa tutafanya mabadiliko” alisema

Prof. Makubi amesema kuwa, vifo vya akina mama wajawazito na mtoto vinaweza kuisha kabisa nchini kama kutakuwa na uwajibikaji na kujitoa kwa kila mtu kwa nafasi yake, ikiwemo uratibu mzuri baina ya watoa huduma za afya ili kuondoa ucheleweshaji wa kupata huduma kwa mama wajawazito, huku akisisitiza kuzitumia Hospitali za kanda kubadilishana ujuzi na hospitali za ngazi ya chini, na utambuzi wa viashiria vibaya kwa mjamzito wakati wa mahudhurio kliniki.

“Kuna njia nyingi mnaweza kutumia ili kushinda hili, ikiwemo kuwawezesha Wataalamu ngazi za chini kuwa na uwezo wa kuzuia hiyo shida, kutoa mafunzo kwa kutumia hospitali za kanda tulizonazo, utambuzi wa viashiria vibaya ambavyo anakuwa navyo mjamzito wakati wa kliniki na uratibu mzuri ili kuondoa ucheleweshaji” alisema Prof. Makubi

Prof. Makubi aliendelea kwa kusisitiza kuwa, katika kuelekea zoezi hili, ni muhimu kuhakikisha utoaji takwimu zilizo sahihi zitakazosaidia kuleta mabadiliko kwa kufanya maboresho katika maeneo mbali mbali ya utoaji huduma.

Mbali na hayo, Prof. Makubi ametoa wito kwa viongozi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro – Mawenzi kwa kushirikiana na Mganga Mkuu wa Mkoa huo kumalizia mradi wa ujenzi wa jengo la mama na mtoto katika Hospitali hiyo, jambo litalosaidia kurahisisha utoaji huduma, hivyo kupunguza vifo vya mama na mtoto.

“Mradi huo wa jengo la mama na mtoto haujamalizika, Serikali inatoa wito mradi huo umalizike kwa wakati, sisi kama Serikali tutafanya kwa upande wetu, ili kuweza kuhakikisha jengo hilo linaweza kukamilika na linaanza kutoa huduma mara moja ” alisema


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527