WAZIRI MBARAWA AFANYA ZIARA KUKAGUA UTEKELEZAJI MIRADI YA MAJI SHINYANGA



Waziri wa Maji Professa Makame Mbarawa, amefanya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji manispaa ya Shinyanga, ambayo inatekelezwa na Wakala wa Maji Safi na usafi wa mazingira vijijini (RUWASA), pamoja na Mamlaka ya Maji na Usafi wa Mazingira Mjini Shinyanga (SHUWASA).


Waziri Mbarawa amefanya ziara hiyo leo kwa kukagua utekelezaji wa mradi wa maji katika kijiji cha Uzogole, Gharamba, pamoja na Mwawaza, ambayo imekamilika kwa asilimia kubwa pamoja na mingine kuanza kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi.

Akizungumza wakati wa ukaguzi wa miradi hiyo ya maji,Waziri Mbarawa amewataka wananchi kutunza miundombinuya maji, ili idumu kwa muda mrefu na kuondokana na adha ya kutotumia tena maji ambayo siyo salama kwa afya zao, pamoja na kupoteza muda wa kufuata maji umbali mrefu huku wakikumbana na changamoto mbalimbali ikiwemo ya wanyama aina ya fisi.

“Naombeni sana wananchi wa Shinyanga muitunze miundombinu ya miradi hii ya maji, ili udumu kwa muda mrefu kuwapatia huduma ya maji safi na salama na muondokane na adha ya kutafuta maji umbari mrefu pamoja na kutumia maji ambayo siyo salama,” amesema Mbarawa.

“Maeneo ambayo kuna mradi na hamjapata maji tutaongeza vituo vya kuchotea maji (BP), ili wote mnufaike na maji safi na salama, lengo la Serikali ni kumaliza kabisa tatizo la maji hapa nchini,” ameongeza.

Katika hatua nyingine, Mbarawa amezitaka mamlaka za maji na wakala wa maji (Ruwasa), kuacha kutumia Wakandarasi kwenye utekelezaji wa miradi ya maji ambayo wanauwezo nayo, bali watumie wataalam wa ndani, (Force Account), ili kupunguza gharama pamoja na miradi hiyo kukamilika kwa wakati.

Kwa upande wake, Kaimu Meneja Wakala wa Maji Vijijini (RUWASA) Julieth Payovela, awali akisoma taarifa ya utekelezaji wa miradi ya maji mkoani Shinyanga , amesema miradi ambayo inatekelezwa na mamlaka za maji na Ruwasa imekamilika kwa asilimia kubwa tofauti na ile ya wakandarasi.

Aidha mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, amemuomba Waziri huyo wa maji, kuongeza nguvu ya ukamilishwaji wa miradi mikubwa ya maji ambayo ipo Masengwa na Mwakitolyo, ili ikamilike haraka na kutoa huduma ya maji safi na salama kwa wananchi.


TAZAMA PICHA HAPA CHINI


Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa, akikagua utekelezaji wa miradi ya maji.

Waziri wa Maji Prof. Makame Mbarawa akizungumza mara baada ya kumaliza kukagua miradi ya maji.


Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, akizungumza mara baada ya kumalizika kwa ukaguzi wa utekelezaji wa miradi ya maji.

Kaimu Meneja Wakala wa maji mjini na vijijini wilaya ya Shinyanga Emmael Nkopi, akielezea utekelezaji wa mradi wa maji katika kijiji cha Gharamba manispaa ya Shinyanga.

Mwananchi Neema Richard, akieleza kufurajishwa na mradi wa maji kijijini kwao Gharamba, ambao utawaondolea changamoto ya kutotumia maji ambayo siyo salama tena kwa afya zao.

Waziri wa maji Prof Makame Mbarawa, akimtiwsha ndoo ya maji mwanamke Kibibi Elias wa kijiji cha Uzogole manispaa ya Shinyanga, mara baada ya kumaliza kukagua mradi wa maji kijijini humo.

Waziri wa Maji Prof Makame Mbarawa, akinawa mikono kwenye mradi wa maji Gharamba.

Awali Prof Makame Mbarawa, akipokea taarifa ya mkoa wa Shinyanga juu ya utekelezaji wa miradi ya maji kabla ya kuanza ziara ya kutembelea miradi hiyo.

Kaimu wakala wa maji mjini na vijijini (Ruwasa) mkoa wa Shinyanga Julieth Payovela, akisoma taarifa ya mkoa juu ya utekelezaji wa miradi ya maji.

Awali Waziri wa maji Prof Makame Mbarawa, kushoto, akisalimiana na Katibu tawala mkoa wa Shinyanga Albert Masovela katikati, pamoja na mkuu wa wilaya ya Shinyanga Jasinta Mboneko, alipowasili mkoani Shinyanga .

Awali waziri wa maji Prof Makame Mbarawa, akiwasili kwenye ofisi za mkuu wa mkoa wa Shinyanga, kwa ajili ya ziara yake ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji.

Waziri wa maji Prof Makame Mbarawa, kushoto akiwa na Katibu tawala wa mkoa wa Shinyanga Albert Msovela, kulia, kwenye ofisi za mkuu wa mkoa wa Shinyanga , alipowasili kwa ajili ya ziara ya kukagua utekelezaji wa miradi ya maji.


Na Marco Maduhu- Shinyanga.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527