RC KUNENGE ATEMBELEA UJENZI WA MIRADI YA DAWASA YENYE THAMANI YA ZAIDI YA SHILINGI BILIONI 100.


Na Azmala Said - Dar es salaam
Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Aboubakar Kunenge amefanya ziara ya kutembelea ujenzi wa miradi mbalimbali ya usambazaji wa Maji jijini humo yenye thamani ya zaidi ya Shilingi Bilioni 100 ambapo amewataka wakandarasi kukamilisha miradi kwa wakati.

Miongoni mwa Miradi aliyotembelea Kunenge ni Ujenzi wa Tank la Lita million 14 linalopokea maji kutoka Visima vya Kimbiji na Mpela lililopo Kisarawe Two lenye thamani ya Shilingi Bilioni 30 ambapo litasambaza Maji kwenye Maeneo ya Wilaya ya Kigamboni.

Aidha Kunenge ametembelea Mradi wa Maji kutoka Kisarawe - Pugu station unaogharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 6.9 ambao utakuwa na uwezo wa kusambaza Lita million milioni 2 kwa zaidi ya wananchi laki nne wa maeneo ya Chanika, Majoe,Ukonga, Buyuni,Gongolamboto,Kigogo na Pugu. 

Kunenge pia ametembelea Mradi wa Uboreshaji Usambazaji wa Maji kutoka Makongo hadi Bagamoyo unaogharimu kiasi cha Shilingi Bilioni 65 unaokwenda sambamba na ulazaji wa Mabomba ya Maji kwa urefu wa Km 1,700.

Kunenge amewasisitiza DAWASA pia kulipatia ufumbuzi tatizo upotevu wa maji huku akiwataka wananchi kuhakikisha wanalipa bili za maji kwa wakati.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa DAWASA Mhandisi Cyprian Luhemeja amesema kuwa Mamlaka hiyo imejidhatiti kuhakikisha tatizo la Maji linabaki kuwa historia kupitia miradi mbalimbali wanayoitekeleza.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527