TASAF YATAMBULISHA ZOEZI LA KUHAKIKI WALENGWA WA MPANGO WA KUNUSURU KAYA MASKINI MANISPAA YA SHINYANGA


Kaimu Mkurugenzi wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini - TASAF Fariji Mishael ametambulisha rasmi zoezi la kuhakiki walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya maskini katika wilaya ya Shinyanga ili kubaini kaya zinazostahili kubaki ama kuondolewa kwenye Mpango wa TASAF Awamu ya III Sehemu ya Pili iliyoanza mwaka 2020.


Akitambulisha zoezi hilo, kwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko Julai 20,2020, Kaimu Mkurugenzi wa TASAF Fariji Mishael alisema wameanza kukusanya takwimu nchi nzima ili kuhakiki walengwa wa TASAF na kwa upande wa wilaya ya Shinyanga zoezi litaanzia katika Manispaa ya Shinyanga.

“Tunasafisha daftari letu ili tuondoe watu wote ambao kwa sasa hawastahili kuwepo katika mpango tuwe na walengwa halisia. Katika zoezi hili tutatoa mafunzo kwa wawezeshaji na watendaji namna ya kufanya kazi na baada ya mafunzo hayo wataanza kukusanya”,alisema Mishael.

Alieleza kuwa wanafanya uhakiki kwa kuzingatia vigezo vya umaskini vilivyoainishwa na taasisi za takwimu za kitaifa ili kuonesha jinsi mpango ulivyofanya kazi vizuri ambapo zoezi hilo linafanyika kwenye halmashauri na wilaya zote zilizopo kwenye Mpango huo.

“Utekelezaji wa TASAF Awamu ya III Sehemu ya Pili umeanza mwaka 2020 itaisha mwaka 2023 ambapo tumeanza kwa kuhakiki walengwa tulionao ili tuwe na walengwa wanaokidhi vigezo”,alisema.

“Wawezeshaji na watendaji waliopo vijijini watakaokwenda kufanya kazi ya kuhakiki watakula kiapo ili wahakiki na kutoa taarifa zilizo sahihi na wale wataonekana wametoa taarifa au takwimu zisizo sahihi zikiwemo halmashauri nazo zitawajibika”,alifafanua Mishael.

Hata hivyo alisema Mpango TASAF Awamu ya Pili sehemu ya kwanza iliyoisha Desemba 2019 umetekelezwa vizuri na kwa mafanikio makubwa na kusaidia kupunguza umaskini katika kaya kwa kiwango kikubwa.

Kwa upande, Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko alisema malengo ya serikali ni kuhakikisha fedha zinazotolewa na serikali zinasaidia wananchi na kwamba serikali inataka kuona walengwa halisi wanaingia kwenye mpango na wale waliopata fedha basi matokeo chanya yaonekane kwa kuboresha maisha ya wananchi.

“Sasa hivi hatutaki kusikia wananchi wakilalamika kusahaulika au kuachwa kwenye mpango,wawezeshaji semeni ukweli kuhusu walengwa,wanaotakiwa waingizwe kwenye mpango, wawe watu wanaostahili na wale walionufaika wasimamieni ili waendelee kuwa katika hali nzuri”,alisema Mboneko.
Kaimu Mkurugenzi wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini - TASAF Fariji Mishael (kushoto) akitambulisha zoezi la kuhakiki walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya maskini kwa Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Mhe. Jasinta Mboneko (kulia) zoezi ambalo linalenga kubaini kaya zinazostahili kubaki ama kuondolewa kwenye Mpango wa TASAF Awamu ya III Sehemu ya Pili iliyoanza mwaka 2020. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Kaimu Mkurugenzi wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini - TASAF Fariji Mishael (kushoto) akitambulisha zoezi la kuhakiki walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya maskini katika wilaya ya Shinyanga.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko akizungumza wakati Kaimu Mkurugenzi wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini - TASAF Fariji Mishael ametambulisha rasmi zoezi la kuhakiki walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya maskini katika wilaya ya Shinyanga ili kubaini kaya zinazostahili kubaki ama kuondolewa kwenye Mpango wa TASAF Awamu ya III Sehemu ya Pili iliyoanza mwaka 2020.

Kushoto ni Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko akizungumza  ambapo alisema serikali inataka kuona walengwa halisi wa TASADF wanaingia kwenye mpango na wale waliopata fedha basi matokeo chanya yaonekane kwa kuboresha maisha ya wananchi.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga, Jasinta Mboneko akizungumza  akihamasisha wananchi wasitumie fedha za TASAF kwa malengo yaliyokusudiwa kama vile kutumia fedha za TASAF kununua pombe.
Kaimu Mkurugenzi wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini - TASAF Fariji Mishael (katikati) akifafanua jambo wakati akitambulisha zoezi la kuhakiki walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika wilaya ya Shinyanga.
Maafisa kutoka TASAF wakiwa katika ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Shinyanga.
Maafisa kutoka TASAF na Wajumbe kamati ya Ulinzi wilaya ya Shinyanga wakiwa katika ofisi ya Mkuu wa wilaya ya Shinyanga.
Picha zote na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527