OFISI ZA ARDHI ZA MIKOA ZATAKIWA KUWA NA DAFTARI LA MIGOGORO YA ARDHI

Na Munir Shemweta, WANMM MANYARA

Wazairi wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ameziataka ofisi za ardhi za mikoa zilizozanzishwa hivi karibuni kuwa na daftari maalum lenye orodha ya migogoro ya ardhi ili kurahisisha ufuatiliaji sambamba na utatuzi wa migogoro kwenye mikoa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Ofisi ya Ardhi ya Mkoa jana mkoani Manyara, Lukuvi alisema kila ofisi ya ardhi ya mkoa inatakiwa kuwa na daftari zuri lenye orodha ya migogoro yote ya ardhi kwenye mkoa husika ikiwa ni mkakati wa kushughulikia migogoro ya ardhi.

‘’Sasa hivi hatutegemei migogoro mipya maana migogoro tunayoshughulika nayo sasa ni ile ya miaka ya nyuma hivyo muorodheshe migogoro yote iliyopo wilayani na kuanza kuishughulikia’’ alisema Lukuvi.

Waziri Lukuvi ameshangazwa na ofisi za ardhi katika halmashauri za wilaya nchini kushindwa kutatua migogoro ya mipaka baina ya wilaya na wilaya wakati halmashauri hizo zina wataalamu wa sekta ya ardhi wanaoweza kuitafsiri GN.

Katika hatua nyingine Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi William Lukuvi ameagiza kufanyika ukaguzi wa mashamba makubwa yaliyomilikishwa kwa wawekezaji kwenye mkoa wa Manyara ili kubaini mashamba yasiyoendelezwa.

Hatua hiyo inafuatia kuelezwa na Mkuu wa mkoa wa Manyara Alexzander Mnyeti kuwa, mkoa huo una mashamba makubwa yasiyoendelezwa kwa muda mrefu wakati uhitaji wa mashamba kwa wananchi wa mkoa huo ni mkubwa kutokana na ongezeko la idadi ya watu.

‘’Hatujatoa ardhi kwa ajili ya kuweka akiba, kazi ya ukaguzi mashamba ni ya kwenu hivyo myaangalie kama yameendelezwa, yana faida gani na yanalipa kodi’’ alisema Waziri Lukuvi.

Kwa upande wake Mkuu wa mkoa wa Manyara Alexzander Mnyeti aliwapongeza watumishi wa sekta ya ardhi katika mkoa wake kwa kufanya kazi kwa utii na nidhamu  tofauti na ilivyokuwa huko nyuma kwa watumishi wa sekta hiyo.

Mnyeti aliongeza kwa kusema kuwa, mkoa wa Manyara umekuwa na tatizo la wananchi kuvamia maeneo ya umma ambapo alisema uvamizi huo unachangiwa na kukosekana hati miliki za maeneo hayo na hivyo kutoa mwanya maeneo hayo kuvamiwa.

Naye Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mary Makondo alisema Wizara yake imefanikiwa katika suala la usimamizi rasilimali ya ardhi huku lengo likiwa kutaka kupima kila kipande cha ardhi na kuwamilikisha wananchi jambo alilolieleza itapunguza migogoro na wakati huo kuiingizia serikali mapato yatokanayo na kodi ya pango la ardhi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527