RAIS MAGUFULI : TUTATUMA NDEGE MADAGASCAR KUFUATA DAWA INAYOTIBU CORONA


Dawa ya mitishamba inayodaiwa kutibu Covid-19 
Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli amesema atatuma ndege kwenda nchini Magascar kuchukua dawa inayodaiwa kutibu ugonjwa wa Corona.

Rais Magufuli ameyasema hayo leo Jumapili Mei 3,2020 wakati akimuapisha Dkt. Mwigulu Nchemba kuwa Waziri wa Katiba na Sheria.

"Nimewasiliana na Madascar na wameshaandika barua wanasema kuna dawa zimepatikana kule,tutatuma ndege kule na dawa zitaletwa pia ili Watanzania nao waweze kufaidika nayo kwa hiyo sisi serikali tupo tunafanya kazi usiku na mchana",amesema Rais Magufuli.

"Wengine wanasema nipo Chato kwani waliambiwa huku Chato sitakiwi kuwepo..huku si ndiko nitazikwa..nikienda Moshi kesho napo watasema nipo Moshi nimekimbia wapi,makao makuu yapo Dodoma lakini hizi ni siasa za kutumia kila kitu ni siasa..hapa ndipo wakati ambao tunatakiwa kusimama pamoja katika kupambana na ugonjwa wa Corona",ameongeza.

Wakati wanasayansi duniani wakihangaika kupata chanjo na tiba ya virusi vya corona, hivi karibuni rais wa Madagascar Andry Rajoelina amezindua dawa ya mitishamba inayotibu' Covid-19 .

Ikizinduliwa kwa jina Covid-Organics, dawa hiyo imetengenezwa kutoka kwa mmea artemisia (pakanga)-ambao ni mojawapo ya miti ambayo huchanganywa pamoja na mimea mingine ya Madagascar kama tiba ya ugonjwa wa Malaria.

Dawa hiyo ambayo imepakiwa kwenye chupa na kutangazwa kama chai ya miti shamba baada ya kujaribiwa kwa watu kadhaa kwa kipindi cha wiki tatu.

Rais Rajoelina aliwataka watafiti kuja na tiba ambayo waliipata kwa muda muafaka

"Vipimo vimefanyika-watu wawili wamekwishapona kutokana na tiba hii," Bwana Rajoelina alisema katika uzinduzi wa Covid-Organics uliofanyika katika taasisi ya utafiti ya Madagascar- Malagasy Institute of Applied Research (Imra), ambayo ndiyo iliyotengeneza dawa hiyo ya mitishamba.

"Kinywaji cha dawa hii ya mitishamba huonesha matokeo katika kipindi siku saba," alisema rais huyo mwenye umri wa miaka 45, ambaye aliwataka watu kuitumia kama hatua ya kujikinga na ugonjwa wa corona.

"Watoto wa shule wanapaswa kupewa kinywaji ... kidogo kidogo kwa siku nzima," aliwaambia mabalozi na watu wengine waliokuwa wamekusanyika kwa ajili ya uzinduzi wa kinywaji hicho.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post