CHINA YAIONYA MAREKANI KUSABABISHA VITA BARIDI ‘MAREKANI IMEAMBUKIZWA NA 'VIRUSI VYA KISIASA'


Waziri wa masuala ya kigeni nchini China ameishutumu Marekani kwa kueneza dhana potofu na uongo kuhusu virusi vya corona hatua inayozua hofu kati ya mataifa hayo mawili.
Marekani imeambukizwa na 'virusi vya kisiasa' vinavyowasukuma baadhi ya wanasiasa kuishambulia mara kwa mara China ,Wang Yi aliambia maripota siku ya Jumapili.

Aliitaka Marekani kuacha kupoteza wakati pamoja na maisha ya watu wasio na hatia katika vita vyake dhidi ya Covid-19.

Hali ya wasiwasi kati ya Washington na Beijing imeongezeka huku virusi hivyo vikisambaa.

Rais wa Marekani Donald Trump , ambaye anakabiliwa na uchaguzi mkuu mwaka huu amekosolewa kwa jinsi anavyopigana vita vyake dhidi ya ugonjwa huo na amelaumu China kwa kujaribu kuficha mlipuko huo.

Lakini siku ya Jumapili, Bwana Wang alirejelea msimamo wa China kwamba taifa hilo lilichukua hatua zilizohitajika kukabiliana na virusi hivyo tangu viliporipotiwa mwezi Disemba.

Je ni nini kingine kilichosemwa na China?

Akizungumza katika mkutano wa kila mwaka wakati wa vikao vya bunge nchini China, bwana Wang alisema kwamba baadhi ya wanasiasa nchini Marekani wanajaribu kuuteka nyara uhusiano wa China na Marekani.

Hakusema moja kwa moja ni wanasiasa gani, lakini akasema wanasukuma mataifa hayo katika hali ya vita baridi.

'Mbali na athari zilizosababishwa na Covid-19 , kuna virusi vya kisiasa vinavyoenea Marekani', aliendelea.

'Virusi hivi vya kisiasa vinachukua kila fursa ya kushambulia na kuiharibia jina China', alisema.

''Baadhi ya wanasiasa hupuuza ukweli uliopo na wamejenga uongo chungu nzima dhidi ya China na kupanga njama nyingi tu''.

Lakini alitoa wito wa ushirikiano kati ya Washington na Beijing katika kukabiliana na virusi hivyo.

''Sote tuna jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa kuna amani duniani na maendeleo'', alisema.

China na Marekani zitafaidika pakubwa kupitia ushirikiano na hasara kubwa kupitia mfarakano.

Je ni nini haswa kinachojitokeza?

Rais Trump na Bejing wamerushiana cheche za maneno katika wiki za hivi karibuni , kuhusu masuala kadhaa katika Shirika la Afya Duniani kwa kuipendelea China katika hatua ya taifa hilo kuficha mlipuko huo kwa mara ya kwanza ulivyoanza kuenea.

Mataifa hayo mawili yenye uwezo mkubwa duniani yamekuwa yakikwaruzana kwa muda mrefu kuhusu masuala ya Biashara na haki za kibinadamu, lakini hali ya wasiwasi imeongezeka maradufu kufuatia mlipuko wa virusi vya corona.

Siku ya Jumapili Bwana Wang alisema kwamba mapendekezo kwamba Marekani huenda ikaichukulia hatua za kisheria China ni ndoto ambayo haitafanikiwa na inayokosa mfano.

Pia aliliteteaWHO na kiongozi wake Tedris Adhanom Ghebreyesus , ambaye amekuwa akilengwa katika ukosoaji wa hivi karibuni.

Wiki iliopita, rais Trump alilishutumu WHO kwa kuwa 'kikaragosi' cha China na kwamba lilisababisha virusi hivyo kutodhibitika kwa gharama ya kupotea kwa maisha ya mengi.

Baadaye alisambaza barua aliotuma kwa Dkt Tedros ambayo ilizungumzia masuala kadhaa ambayo yalikuwa yanaikera Marekani kuhusu hatua za WHO kukabiliana na virusi hivyo.

Dkt Tedros amekubali kuchunguzwa kuhusu jinsi Shirika hilo lilivyokabiliana na mlipuko huo.

Lakini Bwana Wang aliwaambia maripota siku ya Jumapili kwamba China ilikuwa inaliunga mkono Shirika hilo moja kwa moja. Kuunga mkono WHO ni sawa na kuokoa maisha.

Hili ndio chaguo ambalo taifa lolote linaweza kufikiria linafaa kuchagua.

Hakusema iwapo wanasayansi wa kimataifa wataruhusiwa kuingia China kuchunguza chanzo chake.

Je ni zipi shutuma dhidi ya China?

Mlipuko wa virusi hivyo ulianzia katika mji wa China wa Wuhan mwisho wa mwaka jana na uliripotiwa kuanzia katika soko la chakula.

Tangu wakati huo, hatahivyo , wanasiasa wakuu walipendekeza kwamba chanzo chake ni kituo cha utafiti mjini Wuhan kilichokuwa kikiwafanyia utafiti popo.

China imekana madai hayo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527