CHADEMA WAPUUZA MADAI YA SPIKA JOB NDUGAI...."WABUNGE WETU SIO WEZI"


Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimeadhimia kuyapuuzia maagizo ya Spika wa Bunge la Tanzania Job Ndugai, aliyewataka Wabunge wote wa chama hicho ambao hawahudhurii vikao vya Bunge kwa sasa kurudisha posho walizolipwa, ambapo kwa pamoja  wanadaiwa zaidi ya Milioni 110. Ndugai alisema wasiporudisha pesa hizo watahesabika kuwa ni wezi na watakabidhiwa kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ajili ya hatua zaidi.


Taarifa hiyo imetolewa leo Mei, 11, 2020 na Katibu Mkuu wa Chama hicho John Mnyika, wakati akitoa taarifa ya maadhimio ya Kamati Kuu ya chama hicho, ambapo pamoja na mambo mengine kamati hiyo imeadhimia kuwafukuza uanachama Wabunge wake wanne, ambao ni Anthony Komu, Joseph Selasini, David Silinde pamoja na Wilfred Lwakatare. 

"Kamati Kuu ya Chama imejadili madai ya Spika wa Bunge, Job Ndugai kwamba wabunge wa CHADEMA  ni wezi, imeazimia madai ya Spika ni uongo, na Chama kimetoa rai kwa wabunge wa Chadema kutokutekeleza maelekezo ya Spika kwani yanakwenda kinyume na Katiba, sheria na taratibu" Amesema Mnyika


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527