WAZIRI JAFO AWASILISHA MAKADIRIO YA BAJETI 2020/2021 TAMISEMI


Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa Mhe. Selemani Jafo ameliomba bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kuidhinisha kiasi cha shilingi Trioni 7.02 kwa ajili ya utekelezaji wa majukumu katika mwaka wa fedha 2020/2021.

Akiwasilisha hoja hiyo Bungeni jana Jijini Dodoma Mhe Jafo amesema  makadirio hayo  yanahusisha Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa-(OR-TAMISEMI), Tume ya Utumishi wa waalimu, Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Akifafanua zaidi Mhe Jafo amesema kiasi cha shilingi Trilioni 3.8  kitatumika  kwa ajili ya mishahara, Bilioni 851 kwa matumizi mengine na kiasi cha shilingi trilioni 2.29 kitatumika  kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Amesema katika mwaka wa fedha wa 2020/2021 Serikali imepanga kusimamia utawala bora, kukuza demokrasia, ushirikishwaji wa wananchi na Ugatuaji wa Madaraka kwa Umma (D by D)

Ameendelea  kufafanua kuwa Serikali itaendelea kuratibu na kusimamia utekelezaji wa shughuli za utoaji wa Elimu ya Msingi na Sekondari  katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa ikijumuisha utekelezaji wa mpango wa utoaji wa Elimumsingi Bila Ada

Akifafanua zaidi Mhe.Jafo amesema Serikali inampango wa kuratibu ujenzi wa miundombinu ya maeneo ya utawala katika Mikoa, Wilaya, na Halmashauri mpya na za zamani zipatazo 30 ambazo zinatakiwa  kuhamia katika maeneo yao ya Utawala

Kuhusu ujenzi wa  majengo ya utawala na nyumba za viongozi amesema Serikali itaendelea na ujenzi, ukarabati na ukamilishaji wa majengo ya Ofisi na nyumba za makazi ya Wakuu wa Mikoa, Makatibu Tawala wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Makatibu Tawala wa Wilaya, Makatibu Tawala Wasaidizi, Maafisa Tarafa na watumishi waandamizi

Hata hivyo amesema itafanya matengenezo ya barabara zenye urefu wa Kilometa  23,175.11,  Makaravati2, 052 na mifereji ya maji ya mvua  yenye urefu wa 79.9, Ujenzi wa Madaraja 80  yaliyopo  vijijini na mijini ili kuimarisha miundombinu ya barabara nchini .

Kwa upande wa Ujenzi wa Miundombinu ya Barabara Mhe. Jafo amesema Serikali itajenga barabara zenye urefu wa kilometa 35.3 kwa kiwango cha lami na ukarabati urefu wa kilometa 321 kwa kiwango cha changarawe , kukamilisha ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilometa 47.59 kwa kiwango cha lami Jiji la Dar-es-salaam.

Wakati Huohuo Mhe. Jafo amesema Serikali itaanza  ujenzi wa barabara ya Nzasa-Kilungule-Buza,Ulongoni-Bangulo-Kinyerezi  na Magomeni Mapipa- Urafiki na ujenzi wa barabara zenye urefu wa kilometa 11.7 kwa kiwango cha lami katika Halmashauri ya Manispaa ya Kigamboni

Mhe. Jafo amesema katika suala la afya Seikali  itaendelea kujenga miundombinu ya afya  ambapo  kutajengwa  wodi tatu  katika kila Hospitali ya Halmashauri, kuendelea na ujenzi wa  Hospitali  27, ujenzi wa Zahanati 3 katika kila Halmashauri na ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali 67 zilizojengwa.

Aidha  Mhe. Jafo  amesema katika mwaka wa Fedha wa 2020/2021 Serikali imepanga  kutumia shilingi bilioni 42.3 kwa ajili ya ujenzi wa maabara za sekondari ambazo zitajengwa katika kila Halmashauri.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527