KAMBI YA MAREKANI NCHINI AFGHANISTAN YASHAMBULIWA KWA MAKOMBORA


Makombora matano yameipiga kambi ya jeshi la angani la Marekani ya Bagram nchini Afghanistan leo, lakini hakujawa na ripoti za vifo wala majeruhi na mpaka sasa hakuna kundi lolote lililodai kuhusika na shambulizi hilo. 


Shambulizi hilo limetokea wakati serikali ya Afghanistan ikianza kuwaachilia huru wafungwa wa Taliban kutoka gereza la karibu na kituo cha Bagram, kama sehemu ya hatua ya kujenga imani katika mpango wa amani kati ya Marekani na Taliban unaolenga kumaliza karibu miongo miwili ya vita nchini Afghanistan. 

Ujumbe wa kijeshi unaoongozwa na Jumuiya ya kujihami ya NATO umesema kuwa makombora hayo yaliyoilenga kambi hiyo ya jeshi la Marekani yalifyatuliwa leo asubuhi kutoka kwenye gari lililokuwa limeegeshwa katika kijiji kilicho karibu. 

Wafungwa 100 wa Taliban wanatarajiwa kuachiliwa huru leo kutoka gereza moja la karibu na kambi hiyo, baada ya wanamgambo wengine 100 wa kundi hilo kuachiwa jana.

Credit:DW


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527