DC MJEMA AZUNGUMZIA TAARIFA ZA WAGONJWA WA CORONA KUTOROKA HOSPITALI YA AMANA


Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Sophia Mjema amethibitisha kutokea kwa vurugu za wagonjwa waliowekwa katika uangalizi wa maambukizi ya corona katika Hospitali ya Amana wakitaka kutoroka hospitalini hapo na kurejea nyumbani.

Leo asubuhi katika mitandao ya kijamii, ilisambaa sauti ikielezea wagonjwa katika Hospitali ya Amana ambayo ndiyo kituo cha wagonjwa wenye maambukizi ya virusi vya corona wametoroka na wengine kupanda daladala hali iliyozua hofu katika jamii.

Wagonjwa hao wanadaiwa kutoroka hospitalini hapo leo Alhamisi Aprili 23, wakidai kuna msongamano wa wagonjwa wengi huku kukiwa hakuna dawa wala chakula na wao wanaendelea vizuri lakini hawaruhusiwi kurejea nyumbani.

Akitoa ufafanuzi wakati akihojiwa na Kituo cha Televisheni cha ITV, Mjema amesema siyo kwamba wametoroka ila walikuwa wamechoka hawataki kuendelea kukaa hospitalini hapo.

“Kuna wagonjwa walikuwa wamefika pale wakasema wao hawaumwi sana kwa hiyo walikuwa wanataka waruhusiwe, sasa ukifika pale kama una dalili za maambukizi ya corona lazima ukae kwanza uangaliwe, sasa wao hawataki wanataka waruhusiwe walikuwa wanapiga kelele wanataka kuondoka.

“Walikuwa wanasema wanataka kuondoka tufuatilie kwa maaskari wanaolinda hapo. Kama wametoroka kubwa ni kuwafuatilia maana wanajulikana wanapotoka ili wasiende kueneza ugonjwa sehemu nyingine, ni kuwaambia tu wafuatilie maelekezo ya hospitali kwa wale watakaoonekana wagonjwa na watakaokuwa na nafuu waruhusiwe.

“Kama mtu ana viashiria au ana dalili za corona, ana wasiwasi wa kujiona ni mzima. Mimi nawashauri wasiwe wanaamini mambo yanayosemeka huko, wasikilize serikali inavyosema kufanya vurugu sioni kama inasaidia maana kama mtu ana viashiria aende mtaani hata huko mtaani hawakutaki, tunataka tuwaelimishe kwamba wanapoletwa pale si jela ila wanawaangaliwa na kutibiwa kama wameambukizwa,” amesema Mjema.

==>>Msikilize hapo chini


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527