MADAKTARI WAOMBA VIFAA VYA KUJIKINGA NA CORONA


Chama cha Madaktari Tanzania (MAT), kimeiomba Serikali kurefusha matumizi ya dawa kwa wagonjwa wa kisukari, shinikizo la damu, maumivu ya mgongo na misuli ili kupunguza mrundikano wa wagonjwa katika hospitali ikiwa ni juhudi za kupambana na virusi vya Corona.

Akizungumza leo Alhamisi Apirli 02, jijini Dar es salaam Rais wa chama hicho, Dk. Elisha Osati amesema wagonjwa hao wanaweza kupewa dawa na kutumia kwa miezi mitatu.

“Tunaona kuwa wagonjwa wenye magonjwa kama hayo wana hatari zaidi kupata madhara ya virusi vya corona ndio maana tunapendekeza wapewe dawa za muda mrefu ili kuondoa msongamano wa wagonjwa.

“Tunaamini kuwa wagonjwa hao wakibaki nyumbani wanajikinga zaidi, utafiti mdogo tuliofanya unaonesha asilimia 70 ya wagonjwa hao huenda hospitali kwa marudio au kuchukua dawa,” amesema Dk. Osati.

Aidha ameiomba serikali kuhakikisha uwepo wa vifaa vya kujikinga kwa wafanyakazi wa sekta ya afya.

“Tunaomba serikali na wadau wote wa afya nchini kuelewa na kutambua mchango wa watumishi wa sekta ya afya hivyo vitu kama mask N95 ni muhimu sana kwetu ukizingatia idadi ya wagonjwa wa Covid-19 inaongezeka siku hadi siku,”amesema.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527