Tanzia : MWANDISHI WA HABARI ELIYA MBONEA AFARIKI DUNIA

Eliya Mbonea enzi za uhai wake

Mwandishi wa Habari wa Kampuni ya New Habari 2006 Ltd inayochapisha Magazeti ya Mtanzania,Rai, Bingwa na Dimba pamoja na Mtanzania Digital bwana Eliya Mbonea amefariki dunia leo Jumatatu Aprili 6,2020 wakati akiendelea kupata matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam.

Mwenyekiti wa Klabu ya waandishi wa Habari mkoa wa Arusha (Arusha Press Club), Claude Gwandu amethibitisha taarifa za kifo cha Eliya Mbonea alipozungumza na Malunde 1 blog mchana huu.

"Ni kweli ndugu yetu Elia Mbonea ametutoka mchana huu. 
Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Arusha(APC) kinasikitika kutangaza kifo cha mwanachama wake,Eliya Mbonea kilichotokea alasiri ya leo katika Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es salaam",amesema Gwandu. 

Amesema Mbonea ambaye pia alikuwa Katibu Mkuu wa APC kuanzia 2010 hadi 2013 alihamishiwa Muhimbili wiki tatu zilizopita kutoka Hospitali ya Rufaa ya Kanda KCMC mjini Moshi ambako alikuwa akipatwa matibabu tangu Februari 19 mwaka huu.  

"Mwili wa marehemu unatarajiwa kuzikwa Arusha na taarifa zaidi zitatolewa baada ya kukutana na familia yake baadaye leo jioni",amesema Gwandu. 

Mbonea ni miongoni mwa Wanahabari wenye rekodi ya kufika katika Kilele cha Mlima Kilimanjaro mara nyingi zaidi kuliko Wanahabari wote duniani. 

Mungu Ailaze Mahali Pema Peponi Roho ya Marehemu Eliya Mbonea. Amina
Eliya Mbonea ni miongoni mwa Wanahabari wenye rekodi ya kufika kileleni Mlima Kilimanjaro mara nyingi zaidi kuliko wanahabari wote duniani (Pichani akiwa katika kilele cha Mlima Kilimanjaro enzi za uhai wake)

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527