WACHINA 6 WAFIKISHWA MAHAKAMANI KWA KUTOROKA KARANTINI



Baadhi ya raia wa China na wengine wawili walioshtakiwa

Mahakama ya Nakawa Jijini Kampala Uganda, imewashtaki raia 6 wa China baada ya kutoroka kutoka katika moja ya hoteli nchini humo, ambako waliwekwa Karantini.

Hakimu Mkuu wa Mahakama hiyo, Ruth Nabaasa amewataja raia hao kuwa ni Huang Haiguiang, Li Chaochyan, Lin Xiaofang, Qin Shening, Liang Xinging na Huang W, ambapo wameshtakiwa kwa kosa la kutotii agizo la Serikali kukaa karantini kuzuia kusambaa kwa Virusi vya Corona.

Kesi yao imeahirishwa hadi Mei 4 ambapo itatajwa tena kwa ajili ya hukumu, wakati huo Mahakama itakuwa imeshampata mkalimani mzuri wa lugha ya Kichina.

Kulikuwepo na kituko wakati kesi hiyo ikiendelea, ambapo mkalimani aliyekuwepo mahakamani hapo, Michael Zhong aliacha kutafsiri katikati ya maongezi akisema kuwa hakuwa amelipwa kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Wasaidizi wawili wa Wachina hao ambao ni dereva, Abdu Matovu (35) na mkewe, Swabu Nansuna (27) waliokimbia kabla ya siku 14 za karantini kumalizika, nao walikuwepo mahakamani hapo kusikiliza mashtaka yao.

Wawili hao wanashtakiwa kwa kuwasaidia raia wa China kutoroka kutoka karantini, ambapo nao watatolewa hukumu Mei 4.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527