CAG AWASILISHA RIPOTI YAKE YA UKAGUZI KWA MWAKA WAFEDHA ULIOISHIA MWEZI JUNI 30,2019 HUKU IKIIBUA"MADUDU" MBALIMBALI

Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.

Ofisi ya Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa Hesabu za Serikali[CAG]jana April 6,2020  imewasilisha ripoti yake ya ukaguzi kwa mwaka wa fedha ulioishia mwezi Juni,30,2019  ambapo ukaguzi huo ulihusisha taasisi za serikali kuu,mamlaka za serikali za mitaa ,Mashirika ya umma ,miradi ya maendeleo na vyama vya siasa.


Akizungumza na Waandishi wa habari jana April,6,2020 jijini Dodoma Mkaguzi na mdhibiti mkuu wa Hesabu za serikali [CAG] Charles Kichere alisema katika ripoti hiyo  imetoa jumla ya Hati  1082 za ukaguzi ambapo kati ya hizo ,hati zinazoridhisha ni hati 1,017[sawa na asilimia 94%],hati zenye shaka ni 46[sawa na asilimia 4.25%],hati zisizoridhisha saba [0.64%] na   hati mbaya 12[1.11%]


Aidha,Ripoti hiyo ya Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali [CAG]ilibainisha halmashauri 15 ziliwalipa watumishi waliofariki, kustaafu na watoro.

CAG Charles Kichere anasema katika ripoti hiyo kuwa kati ya kiasi kilicholipwa, Sh132.66 milioni yalikuwa ni malipo ya mishahara na Sh34.77 milioni ni makato ya watumishi hao.

“Hatua za haraka zichukuliwe kurejesha Sh167.43 milioni zilizotumika kulipa watumishi hewa,” ameshauri Kichere.

Baadhi ya halmashauri za wilaya hizo na kiwango kilicholipwa kwa watumishi hewa ni; Buchosa Sh14.94 milioni, Korogwe Sh13.5 milioni, Misungwi Sh8.82 milioni, Ngorongoro Sh7.59 milioni, Siha Sh84 milioni, Sengerema Sh9.1 milioni, Ilemela Sh5.5 milioni na Arusha Sh4.13 milioni.

Kuhusu deni la serikali, Mdhibiti na mkaguzi mkuu wa hesabu za serikali [CAG]Charles Kichere amesema kufikia tarehe 30,Juni,2019 lilikuwa Tsh.Trilioni 53.11 ambapo deni la ndani lilikuwa Tsh.trilioni 14.86 na deni la nje ni Tsh.Trilioni 38.24 ikiwa ni sawa ya ongezeko la Tsh.trilioni 2.18[4%] ikilinganishwa na deni la Tsh.Trilioni 50.93 lililoripotiwa tarehe 30,Juni,2018.

Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) Mhe.Naghenjwa Kaboyoka amesema watakaa  na mashirika ambayo yanapuuza mapendekezo ya kamati   na CAG  huku Kaimu mwenyekiti wa kamati ya kudumu ya Bunge ya Serikali za mitaa[LAAC]Mhe.Abdallah Chikota akisema zitaitwa na kuhojiwa halmashauri ambazo zimekuwa zikifanya kwa mazoea.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527