MA - RMO,DMO WAHIMIZWA KUKAGUA VITUO VYA KUTOLEA HUDUMA ZA AFYA KWA AJILI YA CORONA

Na Majid Abdulkarim, Singida

Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), Dkt.Dorothy Gwajima amewataka Waganga wakuu wa Mikoa na Wilaya kutoka maofisini ili waende kukagua vituo vya kutolea huduma za Afya vilivyotengwa na Serikali kwa ajili ya kuwahudumia watu watakaobainika kupata ugonjwa wa COVID-19 (CORONA).


 Dkt.Gwajima ameyasema hayo tarehe 21 machi, 2020 wilayani Ikungi, mkoani Singida wakati akikagua baadhi ya vituo vya kutolea huduma za afya.

Amesema viongozi hao wana wajibu wa kukagua miundombinu ya vituo hivyo ili kuona kama inakidhi vigezo na kisha watume taarifa Ofisi ya Rais TAMISEMI kila siku.

“Kila mjumbe wa Kamati ya Afya wa Wilaya apewe vituo vya kuvifuatilia kila siku kwani ni sehemu mojawapo ya majukumu yake,” amesema na kuongeza:

"Kila mkuu wa kituo ahakikishe amewashirikisha watumishi wote, Kamati ya Afya ya Kituo na Wahudumu wa Afya Ngazi ya Jamii katika kupanga na kutekeleza mikakati ya kupambana na Corona.”

Naibu Katibu Mkuu alikuwa kwenye ziara ya siku mbili katika wilaya za Ikungi na Manyoni mkoani Singida kutembelea vituo vya kutolea huduma za afya ikiwa ni pamoja na kuangalia utayari wa vituo hivyo katika kuwahudumia wananchi pindi wanapokumbwa na majanga mbalimbali likiwemo tishio la ugonjwa wa COVID-19 (CORONA).


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527