ACHOMWA MOTO AKITUHUMIWA KUIBA MAHINDI SHAMBANI KAHAMA


NA SALVATORY NTANDU

Jeshi la Polisi mkoani  Shinyanga linafanya  uchunguzi wa tukio la Mauaji  ya Mwanaume anayekadiriwa  kuwa na umri wa 25-30 ambaye hajafahamika jina wala makazi aliyepingwa na kisha kuchomwa moto na wananchi wenye hasira kali katika Mtaa Mwime Wilayani Kahama akituhumiwa kuiba mahindi shambani.

Kwa Mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Kamanda wa Polisi mkoa wa Shinyanga, ACP Debora Magiligimba ilisema kuwa tukio hilo limetokea Machi 15 mwaka huu majira ya saa 11 alfajiri ambapo wananchi wa Mtaa huo walimkamata  Marehemu akiiba mahindi katika shamba la mmoja wa wakazi wa mtaa huo.

Alisema kuwa baada ya kumkamata wananchi hao walijichukulia hatua mkononi kwa kumpiga na kisha kumchoma moto na kufariki dunia papo hapo na kisha wao kutokomea kusikojulikana.

“Katika eneo la tukio kulikuwa na Mahindi na Baiskeli karibu na mwili wa Marehemu kiashiria kwamba alitumia usafiri huo kubeba Mahindi”,alisema ACP Magiligimba.

Magiligimba alifafanua kuwa Mwili wa Marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji Kahama na chanzo cha tukio hilo ni kuwania mali (Mahindi) na jitihada za kuwatafuta waliohusika na mauaji hayo zinaendelea ili wawezekufikishwa katika vyombo vya sheria.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527