SERIKALI YAWEKA PINGAMIZI KESI YA TUNDU LISSU KUPINGA KUVULIWA UBUNGE


Serikali imemuwekea pingamizi la awali mbunge wa zamani wa Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu katika maombi yake ya kibali cha kukata rufaa kupigania ubunge wake, ikiiomba Mahakama Kuu iyatupe maombi hayo bila kuyasikiliza.


Lissu amefungua maombi hayo jijini Dar es Salaam dhidi ya Spika wa Bunge na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) akiomba kibali cha kukata rufaa katika Mahakama ya Rufani kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu kuhusu suala hilo.

Awali Serikali ilifanikiwa kuishawishi Mahakama Kuu kutupa shauri la awali la mbunge huyo lililofunguliwa na kaka yake, Alute Mughwai aliyekuwa akiomba kibali cha kufungua shauri kutaka amri ya kutengua tangazo la Spika kuwa ubunge wa Lissu umekoma kutokana na utoro na kutojaza fomu za madeni na madili.

Katika uamuzi wake wa Septemba 9, 2019 uliotolewa na Jaji Sirilius Matupa, mahakama ilitupa maombi hayo ikikubaliana na hoja za Serikali kuwa Lissu hakupaswa kufungua maombi ya namna hiyo, bali alipaswa kufungua shauri la kupinga kufanyika kwa uchaguzi mdogo wa kujaza nafasi yake.

Lakini Lissu hakukubaliana na uamuzi wala maelekezo, ndipo akafungua maombi mengine akiomba kibali cha kukata rufaa kupinga uamuzi huo.

Maombi hayo yalipangwa kusikilizwa jana na Jaji Yose Mlyambina, lakini yalikwama baada ya Serikali kuibuka na pingamizi la awali, ikiiomba maombi hayo ya Lissu yatupiliwe mbali, kwa hoja mbili.

Katika hoja hizo, Serikali inadai maombi hayo hayastahili kwa kuwa yanakiuka sheria na kwamba kwa kuwa yako kinyume cha sheria, basi ni ya usumbufu yanayolenga kuharibu taratibu za kimahakama.

Kufuatia pingamizi hilo la awali, mahakama imesimamisha usikilizwaji wa maombi ya Lissu badala yake ikasikiliza kwanza pingamizi hilo la Serikali, huku ikipanga kulitolea uamuzi Aprili 21, mwaka huu.

Uamuzi huo ndio utakaotoa hatima ya maombi hayo ya Lissu, ama kutupiliwa mbali au kuendelea kusikilizwa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527