KESI YA UFISADI NA ULAGHAI INAYOMKABILI WAZIRI MKUU ISRAEL KUANZA MACHI 17,2020


Kesi inayomkabili Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, ambayo ilikuwa inasubiriwa kwa muda mrfeu, inatarajiwa kusikilizwa Machi 17, kwa mujibu wa vyanzo rasmi kutoka nchini humo.

Waziri Mkuu wa Israel anakabiliwa na mashitaka ya ufisadi, ulaghai na uvunjaji wa imani katika kesi tatu tofauti. Tarehe hiyo imetangazwa Jumanne wiki hii na Wizara ya Sheria.

Jumanne wiki hii Benyamin Netanyahu alipokea mwaliko binafsi kutoka mahakama ya Jerusalem. Waziri Mkuu wa Israel anatakiwa afike mahakamani Machi 17, wakati wa ufunguzi wa kesi yake kwa kusomewa mashtaka yanayomkabili.

Mwezi Novemba, Waziri Mkuu alishitakiwa na mwanasheria mkuu kwa kutoa hongo, kufanya udanganyifu na kuwavunja imani raia waliomchagua kuhusiana na kesi tatu tofauti.

Netanyahu ambaye ni kiongozi wa muda mrefu wa nchi hiyo alidaiwa kukubali kuchukua zawadi kutoka kwa wafanyabiashara matajiri na kutoa hongo ili kuweza kuwa katika vyombo vya habari mara kwa mara.

Bw Netanyahu atakuwa Waziri Mkuu wa kwanza katika historia ya Israeli kufikishwa mbele ya mahakama nchini humo.

Kesi hii itaanza wakati mazungumzo ya kisiasa yatakuwa yanaendelea kwa lengo la kuunda serikali mpya. Benyamin Netanyahu amepata ahadi mpya kutoka kwa washirika wake wa mrengo wa kulia ya kumuunga mkono katika hatua hii. Lakini mkataba huu utadumu hadi lini?Kuna hatari kuwa picha za yeye kuwa mahakamani zitamdhofish kisiasa.

Siku ya Jumanne, mpinzani wake mkuu Benny Gantz alisema katika mkutano wa kampeni yake kwamba kuanzia Machi 17, "Netanyahu atajihusisha tu na kesi yake. Hataweza kusimamia masilahi ya raia wa Israeli, "alisema.

Naibu Waziri wa Ulinzi, mwanachama wa Likud, chama cha Benjamin Netanyahu, anaamini, kwa upande wake, kwamba Benjamin Netanyahu anaweza kusimamia kesi yake na kutekeleza jukumu lake kama Waziri Mkuu.

Chaguzi zilizopita zilizofanywa mwezi Aprili na Septemba mwa 2019 zilikifanya chama cha Bw. Netanyahu cha mrengo wa kulia cha Likud kujikuta kwenye njia panda dhidi ya chama Blue na White hali iliyokifanya kushindwa kuunda serikali.

Changamoto za kisheria zinazomkabili Bw. Netanyahu zimekuwa kizingiti katika majadiliano. Amekuwa akisisitiza kuwa mashtaka hayo ni jaribio la mapinduzi dhidi yake.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527