WATU 7 WAKAMATWA MWANZA KWA KUJIFANYA NI MAOFISA WA USALAMA WA TAIFA KUTOKA IKULU


Jeshi la polisi mkoa wa mwanza kwa kushirikiana na vyombo vingine vya  usalama limefanikiwa kuwakamata watu saba kwa tuhuma  za kujifanya maofisa wa usalama wa taifa  kutoka ikulu, ambao hivi karibuni wamekua wakiwatapeli wananchi na baadhi ya watumishi wa serikali katika jiji la mwanza kwa kujifanya wako katika kazi maalum  na kuwajengea hofu ya kiutendaji na kujenga mazingira ya vitendo vya rushwa suala ambalo haliwezi kukubalika na kupewa nafasi katika jamii inayofuata mfumo wa utawala wa sheria. 



Matukio hayo yametokea kati ya  tarehe 27.12.2019  02.1.2020 hasa maeneo ya nyakato wilayani nyamagana, na taarifa zilipopatikana kuwa wanatumia  gari lenye na,T.751 BNL  aina ya toyota Ambulance  ambalo walidai ni sehemu ya msafara wa viongozi wakuu walikamatwa na makachero na wakaendelea kijitambulisha kuwa wao ni maofisa usalama wa taifa  toka ikulu lakini walipohojiwa kwa kina ilibainika ni matapeli wenye lengo la kuwababaisha watu kwa malengo binafsi.

Watuhumiwa waliokamatwa ni:-
  1. Chalanga Wiliam Chalanga, miaka 45, mkazi wa Pasiansi Mwanza na Arusha.
  2. Hamis Seleman mwalimu, miaka 25, huyu ni fundi magari ma hujifanya Bodyguard wa  Chalanga Wiliam Chalanga
  3. Philipo Petro, miaka 35, mkazi wa Usagara Misungwi  pia ni dereva wa Chalanga Wiliam Chalanga.
  4. Elia Vicent Gunda, miaka 30, anadai yeye ni mchungaji wa kanisa la EAGT  lililopo Kisesa, mkazi wa Kisesa,
  5. Hassan Mohamed Juma, miaka 29, mkazi wa Mkolani, fundi wa IT
  6. Selemani Joramu Karanga, miaka 25, anajifanya mlinzi  wa Chalanga Wiliam Chalanga anayejifanya ni afisa mkuu wa Ikulu.
  7. Michael Richard Mazige mkazi  wa Morogoro.
Pia, amekamtwa  tapeli mwingine ambaye alikuwa akiwapigia watu simu na kujifanya  kuwa yeye ni Kamanda wa Polisi mkoa wa Mwanza, mtu huyu baada ya kukamatwa amefahamika kwa jina la Ashery Justol @ Mnazi, miaka 30,  mfipa, mkristo, mkazi wa Igoma Mwanza,  kabla ya kukamatwa alikuwa  akiwapigia simu watu mbalimbali na kuwatumia ujumbe mfupi (sms) baadhi ya watu huku akiwaaminisha kuwa yeye ndiye Kamanda wa polisi mkoa wa Mwanza na kuwaeleza amepatwa na matatizo ya kijamii hivyo kuwataka washiriki kwa kumchangia fedha au vitu  huku akidai mazingira aliyopo hawezi kuongea ila watume pesa au watumie ujumbe mfupi (sms) kuwasiliana nae.

Mtuhumiwa huyu  alichukua picha ya kamanda Muliro  kwenye mtandao yenye sare za jeshi la polisi na kuiweka kwenye profile yake ya whatsapp kisha kuwapigia simu na kuwatumia ujumbe mfupi (sms) kwenye whatsapp. 

Askari walifanya ufuatiliaji wa haraka baada ya kupata taarifa hizo na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa husika. Jeshi la polisi mkoa wa Mwanza linaendelea kuwatahadharisha wananchi kuwa macho na makundi ya matapeli ambao sasa wanaibuka na kutumia majina ya viongozi kutapeli watu.

 Wito wa jeshi ni kuwa wakitilia mashaka  mtu yeyote watoe taarifa haraka polisi ili hatua za haraka zichukuliwe. Watuhumiwa wote watafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo.

Tukio la pili:-

 Mganga wa kienyeji atuhumiwa kumbaka mgonjwa wake

Jeshi la polisi mkoa wa Mwanza limemkamata na linaendelea  kumshikilia mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la Hemed Jumanne, miaka 40, Muha, Muislam, mkazi wa Sengerema, anayedaiwa kuwa mganga wa kienyeji, kwa tuhuma za kumbaka mwanamke mmoja jina limehifadhiwa miaka 32, mchaga, mkristo, mkazi wa Butimba. 

Tukio hilo limetokea tarehe 04.01.2020 majira ya 07:00hrs asubuhi huko mtaa wa Jiwe, kata ya Igogo wilaya ya Nyamagana, hii ni baada ya mhanga kufika kwa mganga tajwa hapo juu kwa lengo la  kupata tiba ya maradhi yanayomsumbua, ndipo mganga aliingiwa na tamaa ya kimapenzi na baadae alimpa dawa za kumpumbaza kisha kumbaka kwa kuweka baadhi ya dawa  za kienyeji kwenye sehemu za siri za mwanaume (mganga) na baadae kuingiza sehemu za siri za mwanamke kama sehemu ya matibabu kitendo hiki cha kikatili cha kubaka  hakivumiliki, ni cha kinyama na ni kosa la jinai. 

Muhalifu huyu atafikishwa mahakamani haraka iwezekanavyo. 

Mhanga ametibiwa hospitali na hali yake inaendelea vizuri. Kwani ameruhusiwa . 

Jeshi la polisi linatoa wito kwa wananchi kujiepusha na makundi ya wahalififu wanaotumia mwavuli wa uganga wa jadi kutapeli watu na kufanya vitendo vingine vya kijinai


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527