BASATA YAMFUTIA USAJILI MSANII DUDUBAYA ...SASA MARUFUKU KUJIHUSISHA NA SANAA


Msanii wa muziki wa Bongo Flava nchini, Dudubaya amefutiwa usajili na baraza la sanaa la Taifa (BASATA) ambapo  baraza hilo pia limetoa onyo kwa taasisi, kampuni na mtu yeyote kutofanya kazi na msanii huyo. Hatua hiyo imekuja baada ya msanii huyo kukataa wito wa baraza hilo.





Dudubaya ambaye jina lake halisi ni Godfrey Tumaini alitakiwa kufika ofisi za Basata leo Januari 7, 2020 saa 4:00 asubuhi baada ya kusambaa kwa video zake kwenye mitandao ya kijamii akizungumzia mambo mbalimbali, ambapo Basata imeeleza ametumia kauli zisizokuwa na maadili wala staha.


Hata hivyo, Dudubaya aliukataa wito huo kwa kulijibu baraza hilo kuhangaikia kwanza na migogoro iliyopo kati ya baadhi ya vyombo vya habari na wasanii ili kuufanya muziki usonge mbele huku maneno aliyoyatumia katika video zake akieleza kuwa ni ya kawaida.

Kutokana na kutoitikia wito huo, Katibu Mtendaji, wa baraza hilo, Godfrey Mngereza katika tamko lake hilo amesema baraza limechukua hatua ya kumfutia usajili wake kuanzia leo Januari 7,2020.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527