Tanzia : MWANZILISHI MSHAURI NA FUNDI MKUU WA RADIO FARAJA MZEE NAMALOWE AFARIKI DUNIA



Noel Ambrose Namalowe enzi za uhai wake



Fundi Mkuu na Mwanzilishi Mshauri wa Kituo cha Matangazo Radio Faraja FM ya Shinyanga Mzee Noel Ambrose Namalowe (81) amefariki dunia leo Jumatano Januari 8,2020. 


Akizungumza na Malunde 1 blog, Mkurugenzi wa Radio Faraja FM Stereo,Anatoly Salawa amesema Mzee Namalowe amefariki dunia leo majira ya saa mbili asubuhi katika Hospitali ya Muhimbili  Jijini Dar es salaam alikokuwa anapatiwa matibabu tangu Desemba 21,2019.

Salawa amesema Mzee Namalowe ameitumikia Radio Faraja tangu ilipoanzishwa mwaka 2001 na alistaafu mwaka 2015 akiwa Fundi Mkuu wa Redio Faraja akarejea nyumbani kwake jijini Dar es salaam.

Amesema Namalowe alikuwa Fundi mitambo na alikaimu nafasi ya Mkurugenzi wakati Radio inaanzishwa na alishiriki kwa kiasi kikubwa kuweka misingi ya radio. 

“Kwa Niaba ya Mhashamu Baba Askofu Liberatus Sangu wa Jimbo Katoliki la Shinyanga ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Radio Faraja Fm Stereo na Timu ya wafanyakazi wa Radio Faraja napenda kuwataarifu kuhusu kifo cha Mzee Nawalowe.Tumepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo cha Mzee Namalowe. Alikuwa Fundi Mitambo Mkuu wa Radio Faraja FM lakini pia Mzee Namalowe alikuwa Mshauri mkuu wa radio, Kabla hatujaanza kurusha Matangazo wakati wa maandalizi ya kituo chetu, alisaidia kuweka sera namna gani kituo cha redio kiwe kwani alikuwa anaijua sera za utangazaji”,ameeleza Salawa. 

“Mzee Namalowe alikuwa mhimili wa radio Faraja, alikuwa msimamizi wa miundombinu na maelekezo ya kitaalamu ya kuanzishwa Redio,alikuwa msaada mkubwa katika hatua zote za uanzishaji Radio,tangu ujenzi wa jengo ,kusimika mitambo na hadi hatua ya kurusha matangazo”,ameeleza Salawa. 

“Awali alikuwa Radio Tanzania kisha Radio Uhuru kama Chief Engineer. Sisi tulimchukua akiwa Uhuru. Kutokana na uzoefu aliokuwa katika kitengo cha utangazaji. Amekuwa mshauri wa Radio ,",amesema. 

Kwa upande wake Emmanuel Msigwa ambaye amewahi kuwa
Meneja Msaidizi wa vipindi na baadaye Meneja wa vipindi kwa takribani miaka 5 Radio Faraja amesema :

RAMBI RAMBI YANGU KWAKO MZEE NAMALOWE...!

Mwaka 2005 mwezi 4 Mzee Namalowe ulinipokea kwa mara ya kwanza nakuja kuripoti kazini Shinyanga, Radio Faraja wakati huo Fred Tunutu akiwa ndiyo Program Manager ningali Kijana kabisa, baadaye nilirithi nafasi ya Tunutu baada ya kuondoka, nikiwa Meneja wa Vipindi ( ambaye kwa wakati huo ndiye alikuwa kama Mkuu wa Kituo) wewe ukiwa Fundi Mkuu na Mshauri Mkuu wa masuala yote ya Uongozi,Fedha, Miradi na hata wakati mwingine ulikuwa Mwalimu!

Ukweli Mzee Namalowe Mosi, uliipenda na kuiheshimu sana Kazi yako,ulikuwa Babu, Baba na Mlezi wa kila mmoja kazini japo ki nafasi Mimi nilikuwa Bosi wako lakini wewe na Dereva witu Mzee Mahalu mlinipa heshima hiyo Siku zote bila ya kujali Umri wangu ambao ulikuwa Sawa na Mtoto wenu ama Mjukuu wako, kuna wakati nilikuwa naona aibu kukutuma kazi kutokana na heshima ya Umri wako lakini Siku zote ulisisitiza nisiogope kukupa kazi" na kuna wakati ulikuwa unaniita kwa kunitania, Mkuu Leo tuna kazi gani?

Ulikuwa Mwasisi wa jina la " Mkuu" baada ya kukuambia najisikia aibu ukiniiita Bosi.!

Nitakukumbuka Sana Mzee Namalowe Sana Sana, ulinifundisha Nidhamu ya kazi,kuipenda na kuijali kazi yangu kuwaheshimu Watu bila ya kujali Umri au Cheo, hakika ulikuwa HAZINA KUBWA KWA KIZAZI CHETU....!!

#LALASALAMABABU
#TUTAONANABAADAYE

Noel Namalowe alizaliwa Desemba 10,1939 Masasi mkoani Mtwara amestaafu rasmi Radio Faraja mwaka 2015 na atakumbukwa kwa mchango mkubwa katika tasnia ya habari nchini Tanzania kwa kuitumikia Radio Tanzania, Radio Uhuru na Radio Faraja Fm Stereo.

Mungu ailaze Mahali pema peponi Roho ya Marehemu Mzee Noel Namalowe. Amina.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post