WALENGWA WA TASAF WAASWA KUFANYA KAZI KWA BIDII ILI KUONDOKANA NA UMASKINI


Mwenyekiti wa bodi ya TASAF, Dr. Moses Kusiluka (aliyevaa shati nyeupe) akikagua baadhi ya bidhaa zinazouzwa na baadhi ya walengwa wa TASAF katika kijiji cha Khusumay
wilayani Karatu kama njia mojawapo ya kujiongezea kipato.
Mwenyekiti wa Bodi ya TASAF Dr.Moses Kusiluka ambaye pia ndiye Katibu Mkuu Ofisi ya Rais-Ikulu ( aliyevaa koti ) akikagua moja ya majengo ya Shule ya Sekondari yaliyojengwa na TASAF katika kijiji cha Khusumay wilaya ya Karatu. 
Nyumba za Walimu na hosteli ya wanafunzi ( picha ya juu na chini ) yaliyojengwa na TASAF katika Shule ya Sekondari ya Khusumay yanaelezwa kuhamasisha wanafunzi kuhudhuria masomo na kupunguza tatizo la mimba kwa watoto wa kike.
Mkurugenzi Mtendaji wa TASAF,Bw. Ladisilaus Mwamanga akifungua bomba la maji kwenye moja ya nyumba zilizojengwa na TASAF katika Shule ya Sekondari Khusumay wilaya ya Karatu Mkoani Arusha. 
Baadhi ya Wajumbe wa Bodi ya TASAF,Wadau wa Maendeleo na Menejimenti ya TASAF akiangalia ujenzi wa daraja linalojengwa na walengwa wa TASAF katika kijiji cha
Nala wilaya ya Karatu mkoani Arusha kwa utaratibu wa Ajira ya muda.
Baadhi ya wajumbe wa Bodi ya Uongozi ya TASAF, Maafisa wa Serikali na Wadau wa Maendeleo wakiangalia ng’ombe wa mmoja ya Walengwa ambao amewapata baada ya kujumuishwa kwenye Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini katika kijiji cha Nala wilaya ya Karatu mkoani Arusha.

Na Estom Sanga- Karatu 

Katibu Mkuu ofisi ya Rais-Ikulu -Dr. Moses Kusiluka ametoa wito kwa Walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini unaotekelezwa na Serikali kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Jamii-TASAF kufanya kazi kwa bidii ili waweze kuondokana na umaskini uliokithiri. 

Dr. Kusiluka ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa Bodi ya taifa ya Uongozi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii-TASAF ameyasema hayo kwa nyakati tofauti alipotembelea na kukutana na baadhi ya walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini na kukagua miradi inayotekelezwa na TASAF katika wilaya ya Karatu mkoani Arusha ambako aliambatana pia na baadhi ya Wajumbe wa bodi . 

Amesema Serikali inatambua changamoto ya Umaskini unaowakabili wananchi ,lakini akasisitiza kuwa ili kuitokomeza changamoto hiyo wananchi wanapaswa
kujituma kwa kufanyakazi kwa bidii na maarifa na kutumia vizuri mazingira wezeshi yaliyowekwa na Serikali kuinua mapato yao. 

Aidha Dr. Kusiluka amehimiza wazazi kutilia mkazo suala la elimu kwa watoto wao ambao amesema Hiyo ndiyo njia ya uhakika ya kujenga jamii bora ya baadaye itakayoleta ukombozi wa kweli wa ujenzi wa uchumi thabiti wa
kaya husika na taifa kwa ujumla huku ikikemea vikali vitendo vyovyote vinavyoathiri maendeleo ya wanafunzi hususani watoto wa kike. 

‘’tumieni vizuri fursa mliyoipata ya kuwa shuleni ili mtimize ndoto zenu za kuwa wataalamu wa fani mnazozitaka katika utumishi wa taifa hapo baadaye’’ alisisitiza Dr. Kusiluka baada ya kukagua nyumba na hosteli ya wanafunzi wa kike katika shule ya sekondari ya Khusumay ambayo
yamejengwa na TASAF. 

Katika hatua nyingine Mwenyekiti huyo wa
Bodi ya taifa ya Uongozi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii- TASAF amesema licha ya mafanikio makubwa yaliyopatikana katika utekelezaji wa Shughuli za Mfuko huo , Serikali imeanza kuchukua hatua madhubuti za kuhakikisha
kuwa Mfuko huo unaendelea kuwa nyenzo muhimu katika kusaidia jitihada za kupunguza umaskini nchini. 

Wakiwa katika kijiji cha Khusumay,Wajumbe hao wa bodi ya taifa ya Uongozi ya TASAF ,walitembelea kaya za baadhi ya walengwa wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini na
kujionea namna walengwa hao walivyofanikiwa kuboresha makazi yao, kununua mifugo hususani mbuzi, ng’ombe ,kuku na nguruwe kwa kutumia ruzuku waliyoipata kutoka TASAF kama njia mojawapo ya kukuza uchumi wa
kaya za Walengwa hao. 

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa
Mfuko wa Maendeleo ya Jamii-TASAF- Bw. Ladislaus Mwamanga ameishukuru serikali kwa kuendelea kuuthamini Mfuko huo na kuridhia utekelezaji wake kuendelea katika sehemu ya pili ambayo amesema imeagizwa kutekelezwa
katika maeneo yote nchini.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527