Picha : SHIRIKA LA PACESHI LAENDESHA MAFUNZO KWA WASAIDIZI WA KISHERIA MKOA WA SHINYANGA



Shirika la linalotoa msaada wa kisheria mkoani Shinyanga Paralegal Aid Centre (PACESHI), limetoa mafunzo ya kuwajengea uwezo wa kisheria wasaidizi wa kisheria 64, kutoka kwenye halmashauri sita za mkoani Shinyanga, ili wakafanye kazi ya kuwahudumia wananchi wa hali ya chini kupata haki zao kwa mujibu wa sheria.


Mafunzo hayo ambayo yatachukua muda wa siku 15, yamefunguliwa leo Desemba 2, 2019 na  Msajili Msaidizi wa watoa huduma za kisheria kutoka mkoa wa Shinyanga Tedson Ngwale, kwenye ukumbi wa mikutano Kahama Super Lodge Mjini Kahama.

Akizungumza kwenye ufunguzi wa mafunzo hayo, Ngwale, amewataka wasaidizi hao wa kisheria wakaitumie vyema elimu watakayopewa kusaidia wananchi wa hali ya chini kupata haki zao, ambao wamekuwa wakidhulumiwa mali kutokana na kutozijua sheria au kukosa fedha za kuweka mawakili kusimamia kesi zao.

Amesema wasaidizi hao wa kisheria wana msaada mkubwa ndani ya jamii hasa wale wa hali ya chini, ambapo wengi wao wamekuwa wakipoteza haki zao kwa sababu ya kutozijua sheria au ukosefu wa fedha za kulipa mawakili, lakini wasaidizi wa kisheria wataweza kuwasaidia kutafuta haki zao mahakamani bila ya kutoa pesa yoyote.

“Naombeni sana wasaidizi wa kisheria mafunzo haya mkayatumie vyema kusaidia wananchi kupata haki zao hasa wa hali ya chini, na msiende kuendekeza masuala ya rushwa, bali wahudumieni vizuri sababu nyie ndiyo msaada wao mkubwa,”amesema Ngwale.

“Pia mzipitie sheria vizuri zikiwamo zile zinazohusu masuala ya ukatili wa kijinsia hasa Sheria ya mtoto ya mwaka (2009), ili mkatokomeze vitendo vya mimba na ndoa za utotoni, kwa kuwasaidia wahanga wa matukio hayo, kuwashitaki wanaowatendea vitendo hivyo na kuwafunga jela,”ameongeza.

Naye Meneja Mradi wa huduma wa msaada wa kisheria John Shija kutoka Shirika la PACESH Shinyanga mjini,amesema mafunzo hayo ni kwa wasaidizi wapya na yanalenga kata ambazo hazikuwa na wasaidizi wa sheria.

Amesema PACESHI  ambao ndiyo wawezeshaji wa mafunzo hayo, wametumia kiasi cha Shilingi Milioni 100.8 kutoa mafunzo kwa wasaidizi hao wa kisheria, ili wakatumikie wananchi wa hali ya chini.

Amesema mafunzo hayo yatawajengea uwezo wa kisheria namna ya kutoa msaada wa kisheria kwa wananchi hususani kwenye masuala ya ardhi, jinai, mikataba, ajira, mahusiano kazini, Sheria ya ndoa, mtoto, mirathi, migogoro ya ardhi,pamoja na vitendo vya ukatili wa kijinsia kwa wanawake na watoto.


Aidha amesema mafunzo hayo yameshirikisha wasaidizi wa kisheria 64 kutoka halmashauri sita za mkoa wa Shinyanga, ambazo ni Kahama Mji, Msalala, Ushetu, Kishapu, manispaa ya Shinyanga pamoja na halmashauri ya wilaya ya Shinyanga, chini ya ufadhili wa mfuko wa huduma za Sheria Legal Service Falility (LSF).

TAZAMA MATUKIO KATIKA PICHA HAPA CHINI

Msajili Msaidizi wa Watoa Huduma za Kisheria  mkoa wa Shinyanga Tedson Ngwale, akizungumza kwenye ufunguzi wa mafunzo ya  kuwajengea uwezo wa kisheria wasaidizi wa kisheria 64, kutoka kwenye halmashauri sita za mkoani Shinyanga. Picha zote na Marco Maduhu - Malunde 1 blog

Meneja mradi wa huduma wa msaada wa kisheria John Shija kutoka Shirika la PACESH Shinyanga mjini, akielezea madhumuni ya mafunzo hayo ya Sheria kwa wasaidizi wa kisheria.

Wasaidizi wa kisheria wakiwa kwenye mafunzo ya kujengewa uwezo wa sheria.

Wasaidizi wa kisheria wakiwa kwenye mafunzo ya kujengewa uwezo wa sheria.

Wasaidizi wa kisheria wakiwa kwenye mafunzo ya kujengewa uwezo wa sheria.

Wasaidizi wa kisheria wakiwa kwenye mafunzo ya kujengewa uwezo wa sheria.

Wasaidizi wa kisheria wakiwa kwenye mafunzo ya kujengewa uwezo wa sheria.

Wasaidizi wa kisheria wakiwa kwenye mafunzo ya kujengewa uwezo wa sheria.

Wasaidizi wa kisheria wakiwa kwenye mafunzo ya kujengewa uwezo wa sheria.

Msaidizi wa kisheria Twaha Kiliza kutoka manispaa ya Shinyanga , akizungumza kwenye ufunguzi wa mafunzo hayo ya sheria.

Msaidizi wa kisheria Yasinta John, kutoka manispaa ya Shinyanga, akielezea namna watakavyo nufaika na mafunzo kupata uelewa mpana wa kisheria kwenda kuhudumia wananchi wa hali ya chini ambao hawazijui sheria ili kupata haki zao za msingi.

Wasaidizi wa kisheria kutoka halmashauri sita za mkoa wa Shinyanga wakipiga picha ya pamoja na Msajili msaidizi wa watoa huduma za kisheria mkoa wa  Shinyanga Tedson Ngwale.

Picha zote na Marco Maduhu- Malunde 1 Blog.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527