MKUU WA MKOA WA KAGERA APIGA MARUFUKU MISHIKAKI


Mkuu wa Mkoa wa Kagera Brigedia jenerali Marco Gaguti, akichangia damu.
Kushoto ni Mkuu wa Mkoa wa Kagera Brigedia jenerali Marco Gaguti akifagia katika soko kuu 
Na Ashura Jumapili - Malunde 1 blog 
MKUU wa Mkoa wa Kagera Brigedia jenerali Marco Gaguti,amewapiga marufuku wanendesha pikipiki (bodaboda ) kuendesha pikipiki bila kuvaa kofia ngumu (Helmet )sanjari na kubeba abiria zaidi ya mmoja (mshikaki ) na badala yake wazingatie sheria za usalama barabarani.

Brigedia Jen. Gaguti,alipiga marukufu hiyo wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya miaka 58 ya uhuru na miaka 57 ya Jamhuri wakati akiongea na wananchi wa Manispaa ya Bukoba wakiwemo waendesha pikipiki Mkoani Kagera.

Alimuagiza kamanda wa jeshi la polisi mkoani humo (RPC ) Revocatus Malimi ,kuhakikisha suala ya kutii sheria bila shuruti lina kuwa endelevu kwa kusimamia sheria na kanuni za usalama barabarani.

Alisema ahakikishe wanasimamia masuala ya leseni za udereva,uvaaji wa kofia ngumu (elements ),kuacha kubeba mishikaki na mwendo kasi.

Alisema akikamatwa bodaboda na kosa la kubeba mishikaki na abiria pia wachukuliwe hatua kwa kuwekwa mahabusu na mambo mengine yaendelee.

"Haiwezekani kumuadhibu bodaboda pekee yake wakati na abiria wanavunja sheria kwa kupanda pikipiki wawili na kutokuvaa kofia ngumu",alisema mkuu huyo wa Mkoa.

Alisema mwezi Novemba mwaka huu walifanya msako kwa mkoa mzima wa kurejesha nidhamu kwa bodaboda pamoja na utii wa sheria bila shuruti.

"Sitaki kuona bodaboda wanabeba mishikaki,wanavunja sheria sa usalama barabarani na kutokuvaa kofia ngumu mimi ndiyo mlezi wenu niko tayari kushirikina na nyie lakini mfuate sheria za usalama barabarani",alisema.

Hata hivyo mkuu huyo wa mkoa alisema endapo bodaboda watajisajili na kutambulika yuko tayari kuwadhamini ili wapewe pikipiki zao na waachane na masuala ya mikataba ili waweze kilipa kidogokidogo.

Mwendesha bodaboda,Abdumajid Almas alisema kuwa suala la mkuu wa mkoa amelipokea vizuri kwa sababu lilikuwa limeshakuwa na changamoto.

Almas alisema kumekuwa na maegesho ya pikipiki ya kiholela bodaboda hawatambuliki ndiyo maana wateja wanalalamika mara kwa mara kuibiwa simu,mikoba vitu mbalimbali ikiwemo na wizi wa bodaboda.

Katika uzinduzi huo mkuu wa mkoa wa Kagera amezindua kwa kufanya usafi maeneo ya soko kuu la Bukoba akiwa na kamati ya ulinzi na usalama mkoa sanjari na kuchangia damu katika hospitali ya rufaa ya Bukoba.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post