WAZIRI WA MAMBO YA NDANI ATOA ONYO KWA CHADEMA ...."TUMEJIPANGA VIZURI KULINDA AMANI NA USALAMA WA NCHI"


Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, amekionya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kuhusiana na msimamo wake wa kujitoa kwenye zoezi la Uchaguzi wa Serikali za Mitaa kwa madai ya kwamba, anadhani mpango huo huenda ukawa na nia ya kuchafua amani.

Waziri Lugola, ametoa kauli hiyo wakati akizungumza jijini Dodoma, ambapo amesema kama Serikali kupitia Jeshi la Polisi, wamejipanga kuhakikisha zoezi zima la uchaguzi linafanyika kwa amani na usalama.

"Nina taarifa kuwa chama kimoja kimejitoa kwenye Uchaguzi, ni imani yangu chama hicho kinaweza kuwa na mipango ya kuvuruga amani ya nchi hii, nitoe onyo hakutakuwa na nafasi ya chama cha siasa kuratibu mipango ya kuvuruga amani, Serikali tumejipanga kutumia nguvu hakuna amani inavurugwa" amesema Kangi Lugola.


Lugola ameeleza hayo leo Ijumaa Novemba 8, 2019 bungeni mjini Dodoma wakati akijibu mwongo wa wabunge wa CCM, Godluck Mlinga (Ulanga) na Richard Ndasa (Sumve) waliohoji sababu Chadema kujitoa katika uchaguzi.

Goodluck Mlinga aliomba mwongozo na kuhusisha  uamuzi wa Chadema kujitoa kushiriki uchaguzi wa Serikali za mitaa, na vurugu zinazojitokeza.

Mbunge huyo amesema Chadema kimekuwa kikisusa kushiriki chaguzi mbalimbali na akataka kujua hatua ambazo Serikali itazichukua dhidi ya chama hicho. Mwongozo kama huo pia uliombwa na mbunge wa Sumve (CCM), Richard Ndassa.

Akijibu miongozo hiyo baada ya kupewa nafasi na mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge, Waziri huyo wa Mambo ya Ndani amesema Serikali haitanyamaza wala kutochukua hatua kwa vitendo vinavyohatarisha usalama na mali za wananchi.

Amesema polisi wamejipanga kuchukua hatua kwa mtu yeyote, vikundi ama vyama vya siasa  vitakavyofanya fujo wakati wote wa mchakato wa uchaguzi wa Serikali za mitaa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527