JAMII ZA WAFUGAJI MSALALA ZAPIGA MARUFUKU KUWAOZESHA WANAFUNZI WA KIKE PINDI WANAPOMALIZA DARASALA SABA



Baadhi ya wanafunzi kutoka jamii za kifugaji wakiwa wanapata maelekezo kutoka kwa mwalimu wao Maximilian Matongo kabla ya kuingia darasani
Mdau wa elimu Patrik Mahona akizungumza na wafugaji(hawapo pichani) katika kikao hicho.

Baadhi ya wazazi walioshiriki katika kikao hicho ambao ni wafugaji katika kata ya Segese.
***
Na Salvatory Ntandu - Malunde 1 blog
Katika jitihada za kuhakikisha mtoto wa kike anapata elimu katika jamii za Wafugaji katika kata ya Segese Halmashauri ya Msalala mkoani Shinyanga, wamepiga marufuku tabia za wazazi kuwaoza watoto wao pindi wanapohitimu darasa la saba ambapo kwa mwaka huu wameanzisha darasa maalumu kwa watoto wa kike 60.

Uamuzi huo umefikiwa jana na wadau wa elimu wa kata hiyo wakiongozwa na Njile Magonji na Patrick Mahona katika kikao maalumu kilichowakutanisha wazazi, walimu na wanafunzi wa jamii za wafugaji na kusema kuwa wameamua kuanzisha darasa hilo gharama zao wenyewe ili kuzuia watoto wakike pindi wanapomaliza darasa la saba.

Wamesema katika jamii zao ndoa nyingi zimekuwa zikishamiri pindi watoto wa kike wamapohitimu elimu ya msingi kutokana na wengi wao kutowathamini watoto wa kike hali ambayo imekuwa ikisababisha kushindwa kupata elimu kutokana na kuolewa hata kama watakuwa wamefaulu kuendelea na masomo.

Wamefafanua kuwa wamekubaliana kwa pamoja kuwa ni marufuku kumwozesha mwanafunzi ambaye yupo chini ya miaka 18 hata kama hajafaulu kuendelea na elimu ya sekondari ili kutoa fursa ya watoto wa kike katika eneo lao kujifunza maarifa mengine ya nyumbani kama vile ujasiriamali na ufundi.

Rehema Komba na Robart Kisimiza ni miongoni mwa wazazi waliopata fursa ya kutoa maoni yao katika kikao hicho ambapo wameshauri kuwepo kwa njia sahihi ya kuwapatia elimu wafugaji juu ya umuhimu wa kumsomesha mtoto wa kike ili kuzuia mimba na ndoa za utotoni zinazofanywa na wazazi wenye tama ya mali.

Maxmilian Matongo ni mmoja wa walimu katika darasa hilo ambapo amesema katika darasa hilo ambalo pia ni kituo cha kufundishia wanafunzi cha Mt. Clement amesema mpaka sasa darasa hilo lina wanafunzi 90 huku wasichana wakiwa ni 60

Amesema mwitikio wa wazazi kuwaandikisha watoto wa kike kupata elimu hiyo kabla ya kwenda sekondari umekuwa ni mkubwa ikilinganishwa na miaka ya nyuma kwani mwaka huu wasichana wengi wameandikishwa kwa wingi hata kuwazidi wavulana.

Katika kikao hicho Wadau hao wa elimu wamechangia zaidi ya shilingi milioni moja kwa ajili ya kuwalipa walimu ambao wanawafundisha wanafunzi hao katika darasa hilo maalumu ambalo linajumuisha watoto kutoka shule mbalimbali katika kata ya Segese.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527