UHAKIKI TAASISI ZA KIDINI NA JUMUIYA ZA KIJAMII KANDA YA ZIWA


Na Mwandishi Wetu, MOHA
WIZARA ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Ofisi ya Msajili wa Jumuiya za Kijamii na Taasisi za Kidini, itaanza kufanya uhakiki wa Jumuiya na Taasisi hizo awamu ya nne. 


Uhakiki huo utahusisha Mikoa ya Kanda ya Ziwa ambayo ni  Mwanza, Geita, Mara, Simiyu, Kagera na Shinyanga kuanzia Oktoba 7-18, mwaka huu. 


Taarifa iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Meja Jenerali Jacob Kingu, ilisema uhakiki katika mikoa hiyo utafanyika kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza. 


“Katika uhakiki huo, Jumuiya na Taasisi husika zinapaswa kuwasilisha nyaraka mbalimbali, huu ni mchakato endelevu ambao unahusisha mikoa yote nchini,” alisema. 


Alisema nyaraka hizo ni cheti halisi cha usajili na kivuli cha cheti hicho, stakabadhi ya mwisho ya malipo ada iliyolipwa hivi karibuni, katiba ya Jumuiya au Taasisi husika. 


Katiba hiyo ni ile iliyopitishwa na Msajili, barua ambayo inathibitisha uwepo wa Jumuiya, Taasisi husika kutoka kwa Afisa Mtendaji wa Mtaa, Kata mahali ilipo ofisi ya Jumuiya, Taasisi, taarifa ya Mkutano Mkuu wa Mwaka na fedha ya mwaka. 


“Fomu ya uhakiki inapatikana katika tovuti ya Wizara hiyo sambamba na kwenye kituo cha uhakiki,” alifafanua. 


Meja Jenerali Kingu alisema taasisi ambazo zitashindwa kuhakikiwa kwa mujibu wa ratiba ya eneo husika zitalazimika kwenda Makao Makuu ya Wizara jijini Dodoma kwa ajili ya uhakiki na kama zitashindwa kufanyiwa uhakiki kwa muda uliopangwa zitaondolewa kwenye Daftari la Msajili. 


Alisema Taasisi za dini na Jumuiya ambazo hazijasajiliwa zinatakiwa kufika wakati wa uhakiki ili ziweze kupewa utaratibu wa kupata usajili.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527