MTUMWA WA KIKOLONI AIBUKA KUHAMASISHA WANANCHI KUJIANDIKISHA


Katika hali isiyokuwa ya kawaida, kijana mmoja anayefahamika kwa jina la Ikuzi Kicheko (Mzalendo Halisi), ameshangaza watu kwa kuvaa mavazi yaliyokuwa yakivaliwa na watumwa enzi za ukoloni, huku akiwa amebeba bango linalohamasisha watu kujiandikisha kwenye daftari la wapiga kura.

Ikuzi Kicheko, amesema lengo kubwa la kufanya hivyo ni kufuatia kuwepo kwa muamko hafifu wa wananchi kwenye zoezi la kujiandikisha, hali iliyopelekea Serikali kuongeza muda wa zoezi hilo.

"Unajua nilivaa yale mavazi ni kuashiria kuwa kama Watanzania, tunawajibu wa kujiandikisha kwenye daftari la kupiga kura ili kuwapata viongozi tunaowahitaji na kuachana viongozi ambao wanafanana na Mfalme Sultani, ambao walikuwa wanaangalia zaidi maslahi yao binafsi na kuwa mfano wa kiongozi mbaya" amesema Kicheko.

Aidha Kicheko ameongeza kuwa, "lengo langu sio kuwaambia watu kuna utumwa, ila ni kuwaambia nenda kajiandikishe kwenye daftari la kupiga kura, epuka kuwa mtumwa nenda kajiandikishe ili upate kiongozi unayemtaka, maanake ni kwamba usipopiga kura utapata kiongozi usiyemtaka".

Kesho Oktoba 17, 2019, ndiyo mwisho wa kujiandikisha kwenye daftari la kupiga kura ili kushiriki uchaguzi wa Serikali za Mitaa utakaofanyika November, 2019.
CHANZO - EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527