RAIS MAGUFULI ATEUA WAKURUGENZI 10 WA HALMASHAURI ZA MANISPAA, WILAYA NA MKURUGENZI WA TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI (NEC)


 Rais wa Tanzania, John Magufuli leo Oktoba Mosi, 2019 amefanya uteuzi wa wakurugenzi watendaji 10 wa Halmashauri za Wilaya na manispaa na kuwahamisha wawili.

Katika uteuzi huo uliofanyika leo Oktoba Mosi, 2019 kiongozi mkuu huyo wa nchi amemteua, Wilson Charles kuwa mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) kuchukua nafasi ya Athuman Kihamia atakayepangiwa kazi nyingine.

Taarifa iliyotolewa na mkurugenzi wa mawasiliano ya Rais Ikulu, Gerson Msigwa inasema Rais Magufuli pia amemteua Kanali Wilbert Ibuge kuwa Balozi na mkuu itifaki wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Inaeleza kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utumishi na Utawala Bora), Kapteni mstaafu George Mkuchika amefanya uteuzi wa makatibu tawala wawili wa Wilaya.

Charangwa Selemani ambaye amekuwa katibu tawala wa Wilaya ya Ilala na Thomas Salala wilaya ya Mtwara.

Wakurugenzi 10 wa Wilaya na manispaa hawa hapa;

Ndaki Muhuli amekuwa mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya walaya ya Siha mkoani Kilimanjaro ambapo awali alikuwa katibu tawala wilaya ya Kitero, Manyara.

Rehema Bwasi amekuwa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Morogoro, kabla ya uteuzi alikuwa katibu tawala wilaya ya Korogwe, Tanga.

Sheillah Lukuba amekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya manispaa ya Morogoro kabla ya uteuzi huo alikuwa katibu tawala wa wilaya ya Ilala, Dar es Salaam.

Mohamed Mavura amekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Kibiti mkoani Pwani ambaye kabla ya uteuzi huo alikuwa ofisa katika makao makuu ya Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi).

Ezekiel Magehema amekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Kyela mkoani Mbeya. Magehema alikuwa ofisa Tarafa wa Malangali, Iringa.

Diana Zacharia amekuwa mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya wilaya ya Butiama, Mara awali alikuwa ofisa tarafa Ukerewe mkoani Mwanza.

Hanji Godigodi amekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe, awali alikuwa ofisa elimu taaluma Mkoa wa Dar es Salaam.

Said Magaro amekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Uyui mkoa wa Tabora. Magaro kabla ya uteuzi alikuwa ofisa tarafa wa Msota, Pwani.

Hawa Mposi amekuwa Mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Malinyi Mkoa wa Morogoro awali alikuwa ofisa tarafa wa Ifakara, Morogoro.

Godwin Chacha amekuwa mkurugenzi mtendaji wa halmashauri ya wilaya ya Rombo mkoani Kilimanjaro ambaye awali alikuwa ofisa Tarafa wa Maswa, Simiyu.

Wakurugenzi watendaji waliohamishwa vituo vya kazi ni aliyekuwa mkurugenzi mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro amehamishiwa Wilaya ya Itigi mkoani Singida na aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Kibiti mkoani Pwani, Advera Ndebabayo amepelekwa Wilaya ya Arusha.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527