Na Esther Macha - Malunde 1 blog Mbeya
Wanawake watatu Mkoani Mbeya wanashikiliwa na jeshi la polisi kwa tuhuma za kughushi nyaraka mbalimbali kwa lengo la kupata mkopo katika Benki ya Posta Tawi la Mwanjelwa mkoani hapa .
Akizungumza na waandishi wa habari leo Kamanda wa Polisi Mkoani Mbeya, Ulrich Matei alisema kuwa watuhumiwa hao wamekamatwa Septemba 19 mwaka huu majira ya saa 10 jioni katika Benki ya Posta iliyopo katika maeneo ya mwanjelwa mkoani Mbeya.
Alisema kuwa polisi walipata taarifa kutoka kwa raia mwema kuwa watuhumiwa wameghushi majina yao halisi kwa lengo la kupata mkopo kwa njia ya udanganyifu na kukwepa kuonekana kuwa wanadaiwa na taasisi nyingine za kifedha.
Kamanda Matei aliwataja watuhumiwa hao kuwa ni Farida Yessaya (23) Mfanyabiashara na Mkazi wa Uyole ambaye ametengeneza nyaraka zake kwa kutumia jina la mtoto wake mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu aitwaye Caren Zabron, Asha Namwene, (25)Mfanyabiashara na Mkazi wa Uyole ambaye ametengeneza nyaraka zake kwa kutumia jina la mama yake mzazi ambaye ni marehemu aitwaye ,Zaituni Bakili, Rebeka Yessaya (47).
Mfanyabiashara na Mkazi wa Uyole ambaye ni Mwenyekiti wa Kikundi na alithibitisha majina hayo huku akijua sio majina yao halisi waliyotumia kuchukua mkopo katika taasisi ya fedha - FINCA.
Matei alisema watuhumiwa kwa pamoja waliomba mkopo wa shilingi milioni mbili na laki tano [2,500,000] na walitegemea kupewa mkopo huo tarehe 19.09.2019 ila kabla ya kupewa fedha hizo Jeshi la Polisi liliweza kubaini kuwa watuhumiwa wametumia majina yasiyo yao ili kukwepa kurejesha fedha hizo.