NI FURSA NYINGINE TENA KWA WAFANYABIASHARA WA TANZANIA

Na Paschal Dotto-MAELEZO
Baada ya tukio kubwa la Maonesho ya biashara ya kimataifa (sabasaba), yakifuatiwa na Maonesho ya Wiki ya Viwanda ya Nchi za Kusini mwa Afrika (SADC), sasa Tanzania inaenda kuandika historia nyingne katika sekta ya Biashara na uwekezaji kwa Kongamano kubwa la Wafanyabishara wa Tanzania na Uganda kukutana Septamba 6-7, 2019, Katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Julius Nyerere (JNICC).



Matukio hayo ya muhimu yenye sura za kimataifa yametokea ndani ya miezi miwili tu na hili linaloangazwa na wafanyabiashara, wajasiriamali na hata wapanga program za uchumi nchini hili la Tanzania na Uganda litafunguliwa na Wakuu wa Nchi zake mbili.

Mnamo Julai 13, 2019, Dkt John Pombe Magufuli, Rais wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, alimpokea Rais wa Jamhuri ya Uganda, Yoweri Kaguta Museveni akitokea nchini Afrika ya Kusini na kuwa na mazungumzo na hatimaye kufanya mkutano wa hadhara wilayani Chato, Mkoani Geta.

Mkutano huo ulitawaliwa na maada za kuimarisha uchumi wa nchi hizo mbili, miongoni mwao ikiwemo kuimarisha biashara na uwekezaji na kuwakaribisha wafanyabiashara wa Uganda kuja kuwekeza nchini Tanzania.

“Nchi zetu zinafaidika vizuri kiuchumi katika mahusiano yetu, kwani mwaka 2018, biashara kati ya Tanzania na Uganda zilikuwa kwa Shilingi bilioni 358.697 kutoka shilingi bilioni 178.191, mwaka 2015”, Alisema Dkt. Magufuli huku akionyesha kuwa ni mwanzo mzuri.

Katika matumaini hayo, Rais Magufuli akaendelea kusema, “ lakini pia waganda wana miradi 22 ya uwekezaji yenye thamani ya dola za kimarekani bilioni 143.25 ambayo imetoa ajira 2,230.”

Rais Magufuli aliweka wazi kuwa ukarabati wa reli ya kati, upanuzi wa Bandari Kuu ya Dar es Salaam, ufufuaji wa meli ya mizigo ziwa Victoria na ubadilishaji wa baadhi ya masharti katika vituo vya kupima vitawezesha kurahisha usafirishaji wa mizigo ya wafanyabiashara kutoka Uganda.

Mabadiliko mengi ya mifumo ya uendeshaji wa bandari nchini na uboreshaji kwa viwango vikubwa vinaongezea fursa ya ufanisi, na vivyo kumpa matumaini Dkt Magufuli kupokelewa ushawishi wake na Rais Museveni kwa kuwaambia wafanyabiashara wa Uganda kutumia bandari ya Dar es Salaam.

Kufuati Rais Museveni kuitika ombi la ziara hiyo, Dkt John Pombe Magufuli sasa amemualika Rais Museveni kuzindua kongamano la kwanza la biashara kati ya Tanzania na Uganda Septemba 6-7, 2019, JNICC jijini Dar es Salaam.

Katika Mkutano wake na Waandishi wa Habari uliofanyika Septemba 1, 2019, Waziri wa Viwanda, Innocent Bashungwa, alieleza kuwa kongamano hilo litahudhuriwa na wafanyabishara pamoja na watendaji waandamizi wa serikali za pande zote kutoka Tanzania na Uganda.

Tanzania na Uganda zimekuwa kwenye mahusiano imara huku yakijenga uimarishaji wa uchumi, hasa katika sekta ya biashara, uwekezaji na usafirishaji, na kwa fursa hiyo Rais Museveni ataambatana na wafanyabiashara kutoka nchini kwake kukutana na wenzao wa Tanzania.

Kongamano hilo ni fursa kwa watanzania wote wenye biashara na lengo lake likiwa ni kutangaza fursa na kuhamasisha biashara na uwekezaji zilizoko Tanzania na Uganda, pia Serikali itapata fursa ya kuongea na wafanyabiashara hao ili kuangalia changamoto za kufanya biashara katika nchi hizo mbili.

Katika kuimarisha biashara kati ya Tanzania na Uganda Serikali zote mbili zitashirikiana kuangalia fursa na changamoto zilizopo, kubuni mbinu za kuzitatua ili kuongeza biashara katika nchi hizo mbili na kuhamasisha uwekezaji kwa lengo la kukuza uchumi wa nchi zao.

“Sisi Tanzania tumekuwa tunawauzia chakula na vifaa vya viwandani, na kwakuwa tunajenga uchumi wa viwanda, ni fursa kwa watanzania kushiriki kwenye kongamano hilo ambalo litakuwa na tija kubwa kwetu kama nchi, Rais wetu analeta Wakuu wa nchi mbalimbali ikiwemo Uganda ili kuwaonesha fursa tulizonazo pamoja na kujenga mtandao mpana wa biashara”, alisisitiza Bashungwa, Waziri wa Viwanda na Biashara.

Wafanyabiashara wote nchini imeshauriwa wajitokeze na kujipanga kwa bidhaa zao walizonazo na kuwa kongamano hilo ni kubwa na la kipekee kuwahi kutokea kati ya nchi hizo mbili.

Waandaaji wanasema onesho litaambatana na Maonesho ya makubwa ya bidhaa za Tanzania ambapo Watanzania watapata fursa ya kuonesha bidhaa za kilimo na za viwandani, na jinsi Taasisi za umma na sekta binafsi zinazosaidia kuongeza thamani ya mazao kwa kuhimiza minyororo ya thamani.

Kadhalika ujio huo toka Uganda ni fursa ya kuunganisha na kukuza nguvu za umoja kwa wafanyabiashara wa Tanzania na wa Uganda kujenga kasi ya wigo wa biashara, kupata masoko mapya pamoja na kutatua changamoto na kujenga mazingira mazuri zaidi ya kufanya biashara.

Wazalishaji wa bidhaa za kilimo, wadau wa kilimo wakiwemo wafanyabiashara na wamiliki wa viwanda wa jiji la Dar es Salaam na mikoani nchini wanahimizwa kushiriki.

“Wafanyabiashara waelewe kuwa ni mwanzo mzuri wa kupenya katika soko la Sudani ya Kusini kwa sababu wapo wafanyabiashara wa Uganda wanafanya biashara nchini Sudani ya Kusini, ” Waziri Bashungwa.

Mwelekeo wa Serikali ya Awamu ya Tano ni kujenga uchumi wa viwanda, hivyo ni fursa kwa Watanzania kutumia kongamano hili kwasababu Serikali inazidi kuweka mazingira wezeshi ya kufanya biashara nchini, kujenga viwanda na kufuatilia masoko mbalimbali lengo ni kutaka uuzaji wa bidhaa nchini Uganda na nchi zingine ambazo ni jirani na Tanzania.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527