DPP ATOA MUONGOZO KUHUSU WAHUJUMU UCHUMI WANAOTAKA KUSAMEHEWA


Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP), Biswalo Mganga amesema ofisi yake ipo tayari kutekeleza ushauri wa Rais  Magufuli aliyetaka kusikilizwa kwa mahabusu wanaokabiliwa na makosa ya uhujumu uchumi iwapo watakuwa tayari kukiri na kurejesha fedha za serikali wasamehewe.

Mganga amesema jambo hilo linawezekana endapo mshtakiwa mwenyewe ataiandikia ofisi yake barua kupitia kwa Mkuu wa Gereza na kusisitiza kuwa barua hiyo inapaswa kuandikwa na mtuhumiwa mwenyewe aliye gerezani na siyo wakili. .

“Utaratibu ni kwamba, mtuhumiwa mwenyewe aliyeko mahabusu anatakiwa aniandikie barua kupitia kwa mkuu wa gereza akikiri kosa na kuomba kutubu haraka iwezekanavyo na sisi tutachukua hatua.

 “Ni mtuhumiwa mwenyewe ndiye anatakiwa kuandika barua, siyo wakili. Unajua wakili anaweza kubadilika na hata mtuhumiwa kumkana kuwa sijamtuma afanye alichofanya kwa niaba yangu, ndiyo maana mara zote watuhumiwa wanaoomba msamaha na kukiri huandika barua wenyewe kwa mkono wao kupitia kwa mkuu wa gereza” Amesema DPP Mganga.

Akizungumza jana wakati wa kuwaapisha baadhi ya viongozi aliowateua, Rais Magufuli alimuomba DDP ndani ya siku saba kuangalia uwezekano wa kusamehewa baadhi ya watuhumiwa waliokaa muda mrefu mahabusu kwa makosa ya uhujumu uchumi endapo watatubu, akisema anatamani kuona Watanzania wote wanaishi huru ili kushiriki ujenzi wa taifa.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527