ATUPWA JELA MIAKA 60 KWA KUVUTISHA BANGI WATOTO NA KUWALAWITI

Mahakama ya Wilaya ya Musoma mkoani Mara, imemhukumu Nyamasheki Malima (41), kifungo cha miaka 60 jela, kwa kumkuta na hatia ya kuwavutisha bangi watoto wawili wa kiume wenye umri wa miaka 11 na 13 wa familia moja, kisha kuwalawiti.


Akisoma hukumu hiyo mwishoni mwa wiki, Hakimu Jacob Ndira amesema kuwa Malima alitenda makosa hayo kati ya Septemba 2017 na Septemba 2018, baadaye alikamatwa na kufikishwa mahakamani na kusomewa mashtaka yanayomkabili, lakini alikana kufanya kitendo hicho.

Awali, Baba wa watoto hao, ndiye alikuwa mtu wa kwanza kubaini hali hiyo kwa mtoto mmoja wapo akiwa katika hali isiyo ya kawaida, baada ya kumfanyia uchunguzi na kuwahoji ndipo walimtaja mtuhumiwa ambaye alikuwa anawafanyia vitendo hivyo.

Hakimu Ndira, amesema mahakama ilisikiliza maelezo ya ushahidi wa pande zote mbili na kuridhika bila ya kuacha shaka yeyote huku mshtakiwa akijitetea mwenyewe.

Kwa mujibu wa majibu ya vipimo yaliyotolewa na daktari aliyewafanyia vipimo watoto hao, unaonesha kuwa sehemu za haja kubwa zilikuwa zinaingiliwa kila wakati baada ya kuwavutisha bangi watoto hao ambao ni wanafunzi wa shule ya msingi.

Kutokana na maelezo ya kina ya kitabibu ya daktari, hakimu Ndira amesema mahakama imejiridhisha watoto walileweshwa bangi na kulawitiwa.

Hakimu alipo muuliza mshtakiwa kama ana chochote cha kujitetea kwanini mahakama impunguzie adhabu, yeye alidai hana nguvu za kiume hivyo asingeweza kufanya kitendo hicho na kuiomba mahakama imsamehe.

Baada ya utetezi wake Hakimu Ndira alimwambia mtuhumiwa hana namna ya kupunguziwa adhabu, hivyo atakwenda jela miaka 60 kutokana na makosa mawili ya kuwavutisha bangi na kulawiti watoto.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527