MKURUGENZI TPDC ALIYERUDISHWA KAZINI NA RAIS MAGUFULI AACHIWA HURU NA MAHAKAMA


Vigogo watano wa Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC),akiwemo Mkurugenzi Mtendaji wa shirika hilo,James Mataragio wameachiwa huru leo August 19, 2019 katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya Mkurugenzi wa Mashitaka(DPP) kutokuwa na nia ya kuendelea na Mashitaka dhid yao.


Mataragio na wenzake walikuwa wakikabiliwa na shtaka moja la matumizi mabaya ya madaraka ambapo ilidaiwa kati ya Aprili 8, 2015 na Juni 3, 2016 walitenda kosa hilo wakiwa watumishi wa umma na waajiriwa wa TPDC.

Agosti 24, 2016 Bodi ya Wakurugenzi wa TPDC, ilimsimamisha Mkurugenzi huyo kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizokuwa zikimkabili .

Hata hivyo, Julai 22, 2019 Rais Magufuli aliielekeza wizara ya nishati kumrejesha ofisini  katika wadhifa wake aliokuwa nao kabla ya kusimamishwa na kushtakiwa. 

Wengine waliofutiwa mashtaka ni George Seni, aliyekuwa Kaimu Meneja wa Uvumbuzi; Welington Hudson, aliyekuwa Mkuu wa Kitengo cha Manunuzi na Utawala; Kelvin Komba, aliyekuwa Mkurugenzi wa Mkondo wa Juu na Edwin Riwa aliyekuwa Kaimu Mkurugenzi wa Mipango

Wakili wa Serikali Mwandamizi Wankyo Saimoni amedai leo Jumatatu Agosti 19,2019 mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam, Kelvin Mhina kuwa shauri hilo limekuja kwaajili ya kusikilizwa lakini Mkurugenzi wa Mashtaka (DPP) ameonyesha nia ya kutoendelea na kesi hiyo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527