MWAKYEMBE APONGEZA VYOMBO VYA HABARI KWA KUTANGAZA VYEMA MKUTANO WA 39 WA SADC

Na Shamimu Nyaki WHUSM- DODOMA

Waziri wa Habari Utamaduni Sanaa na Michezo Mhe. Dkt. Harrison Mwakyembe amevipongeza Vyombo vya Habari nchini kwa kazi kubwa ya kiuzalendo na weledi wa hali ya juu katika kutangaza Mkutano wa 39 wa Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) uliomalizika jana Jijini Dar es Salaam.

Dkt. Mwakyembe ametoa pongezi hizo jana Jijini hapo ambapo amesema kuwa uandishi wa habari wa kujenga na kukosoa ambao una lengo la kurekebisha unahitaji kupongezwa kwakua unasaidia jamii na Serikali katika kuleta maendeleo ya haraka kwa Taifa.

“Waandishi wa habari mbali na kuutangaza Mkutano wa 39 wa SADC lakini pia wametumia taaluma yao kutangaza fursa za uwekezaji zinazopatikana hapa nchini kupitia sekta mbalimbali ikiwemo Uwekezaji katika viwanda, Utalii, Uchukuzi na nyinginezo,” alisema Dkt. Mwakyembe.

Ameongeza kuwa Uwenyekiti wa Tanzania ambao unaendeshwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Dkt.John Pombe Magufuli umeleta ari na matumaini mapya ambayo yatasaidia nchi wanachama kuondoa vikwazo vingi vya kibiashara na mawasiliano ya karibu baina ya nchi wanachama  na kujenga ustawi wa uchumi kwa nchi hizo.

Aidha Mhe. Mwakyembe  amesema kuwa baada ya lugha adhimu ya Kiswahili kutangazwa rasmi kuwa miongoni mwa lugha nne zinazotumika ndani ya Jumuiya hiyo, amewataka Watanzania kutumia fursa hiyo kutangaza bidhaa za lugha hiyo ikwemo uandishi wa vitabu vya kiada, ufundishaji wa lugha hiyo, kuuza Sanaa zinazotokana na lugha hiyo kwa nchi wanachama wa jumuiya hiyo.

Mkutano wa Jumuiya ya Kusini mwa Afrika SADC kwa Wakuu wa nchi na Viongozi wa Serikali umefanyika kuanzia Agosti 17- 18,2019 ambapo mambo mbalimbali yanayohusu nchi hizo yalijadiliwa ikwemo namna bora ya kuimarisha biashara ndani ya nchi hizo  ambapo Tanzania imeteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo kwa kipindi cha mwaka mmoja kuanzia mwezi Agosti mwaka huu.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527