GIBRALTAR YAKATAA OMBI LA MAREKANI LA KUIZUIA MELI YA IRAN


Gibraltar imepinga ombi la Marekani kuikamata tena meli ya mafuta ya Iran ambayo ilikuwa ikiizuia tangu mwezi Julai kwa kudhania kwamba ilikuwa ikisafirisha mafuta Syria.

Marekani iliwasilisha ombi la mwisho siku ya Ijumaa , siku moja baada ya Giraltar kuiachilia meli hiyo ya Grace 1.

Gibraltar imesema kwamba haikuweza kukubali ombi la Marekani kuikamata tena meli hiyo kwa kuwa vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran havina nguvu Ulaya.

Meli hiyo tayari imeondoka Gibraltar kulingana na mjumbe wa Iran nchini Uingereza.

Tehran imesema kwamba iko tayari kuyapeleka majeshi yake kuisindikiza meli hiyo ambayo jina lake lilibadilishwa kutoka Grace 1 hadi Adrian Drya 1.

Meli hiyo na wafanyakazi wake 29 kutoka India, Urusi, Latvia na Ufilipino ilikamatwa kupitia usaidizi wa wanamaji wa Uingereza tarehe 4 Julai baada ya serikali ya Gibraltar - eneo linalomilikiwa na Uingereza kusema kwamba ilikuwa ikielekea Syria hatua inayokiuka vikwazo vya Muungano wa Ulaya.

Hatua hiyo ilizua mgogoro wa kidiplomasia kati ya Uingereza na Iran , ambao umeendelea katika wiki za hivi karibuni huku Iran nayo ikiikamata meli iliokuwa ikipeperusha bendera ya Uingereza Stena Impero katika Ghuba.

Mamlaka ya Gibraltar iliiwachilia meli hiyo siku ya Alhamisi baada ya kupokea hakikisho kutoka Iran kwamba haitaipeleka mafuta yake nchini Syria.

Idara ya haki nchini Marekani baadaye ikawasilisha ombi mahakamani la kuizuilia meli hiyo kwa msingi kwamba ina uhusiano na jeshi la Iran ambalo imelitaja kuwa kundi la kigaidi.

Gibraltar , katika taarifa yake siku ya Jumapili ilisema kwamba haikuweza kukubali ombi hilo kwa kuwa jeshi hilo la Revolutionary Guard sio kundi la kigaidi kulingana na EU ambalo eneo hilo la Uingereza ni mshirika wake.

Pia ilisema kwamba vikwazo vya Marekani vya kuzuia uuzaji wa mafiuta wa Iran haviwezi kuidhinishwa na EU ikidai tofauti iliopo kati ya Marekani na EU kuhusu Iran.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527