SERIKALI YATOA BILION 5.7 UJENZI WA MAABARA NA JENGO LA UPASUAJI – SIMIYU


Na WAMJW- SIMIYU
Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia,Wazee na Watoto yatoa kiasi cha shilingi Bilion 5.7 kwaajili ya ujenzi wa jengo la maabara na jengo la upasuaji ikiwa ni awamu ya pili, baada yakuzinduliwa kwa awamu ya kwanza na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt John Pombe Magufuli, Mwezi Agasti 2018.


Hayo yamesemwa  jana na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Ummy Mwalimu wakati alipofanya ziara ya kukagua mradi wa maendeleo ya ujenzi wa jengo la maabara na jengo la upasuaji katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu.

Waziri Ummy amesema kuwa, uwekezaji huu umeweka alama kubwa kwa Serikali ya awamu ya tano inayoongozwa na Mhe. Rais Dkt.John Pombe Magufuli kwa kuwasogezea huduma bora zakibingwa kwa Wananchi wa Simiyu jambo litalosaidia kuondoa usumbufu katika kutafuta huduma hizo.

“Kipekee kabisa nimshukuru Mhe. Rais katika mwaka huu 2018/2019 ameipatia Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Simiyu kiasi cha shilingi Bilion 5.7 kwaajili ya ujenzi wa jengo la maabara na jengo la upasuaji lakini pia litakuwa na huduma za mionzi” alisema Waziri Ummy.

Aidha, Waziri Ummy ameongeza kuwa Serikali tayari umeshapata kiasi cha shilingi Bilion 2.2 kwaajili ya ujenzi wa jengo la mama na mtoto ili huduma za kulaza Wagonjwa zianze kutolewa katika Hospitali hiyo.

“Tuna pesa nyingine kiasi cha shilingi Bilion 2.2 ukiacha zile Bilion 5.7 tutaanza kujenga jengo la mama na mtoto ili sasa tuanze kulaza wagonjwa, kwasababu ukiangalia wagonjwa wengi ni Wanawake na Watoto, lakini hili kingine la wodi nyingine nalibeba pia” alisema Waziri Ummy.

Mbali na hayo, Waziri Ummy amewaagiza Watumishi wa Sekta ya Afya kuzingatia maadili na weledi wa kazi zao ikiwemo matumizi mazuri ya lugha kwa wagonjwa pindi wakiwa kupata huduma za Afya.

“Niinawataka tena Wauguzi kuzingatia maadili na weledi wa kazi zao ,ikiwemo kutumia lugha nzuri, lugha yenye busara na lugha yenye upendo kwa wagonjwa, asili ya muuguzi ni upendo na heshima na kumthamini mtu ambae unampa huduma ” amesema Waziri Ummy.

Hata hivyo, Waziri Ummy aliendelea kusema kuwa Serikali haitokuwa na msamaha na Mtumishi yeyote ambae atabainika ametoa lugha chafu kwa wagonjwa ikiwemo kujihusisha na masuala ya Rushwa kwa kuwachukulia hatua kali ikiwemo kufuta reseni zao.

Nae Mkuu wa Mkoa wa Simiyu Mhe. Anthony Mtaka amesema kuwa changamoto kubwa ambayo itakuwepo katika ujenzi wa Hospitali hiyo ni uwepo wa wodi, hivyo amemwomba Waziri Ummy kuharakisha ujenzi wa wodi ili huduma zianze mara moja.

“Wakati wote tunapokuwa tunakuja changamoto kubwa ilikuwa ni wodi, na hata wagonjwa wanaokuja wanaulizia kuhusu wodi za kulala wagonjwa ” amesema Mhe. Mtaka.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527