TAKUKURU KAGERA YATOA ONYO KALI KWA VIONGOZI WA VYAMA VYA SIASA

Katika kuelekea uchaguzi wa serikali za mitaa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) mkoa wa Kagera imetoa tahadhali na onyo kali kwa viongozi wa vyama vya siasa ambao ni wagombea watakaojihusisha na vitendo vya rushwa.


Kauli hiyo imetolewa na mkuu wa TAKUKURU mkoani Kagera John  Joseph wakati akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana Julai 13,2019.

Joseph amesema vitendo vya rushwa bado ni tatizo kwa baadhi ya watumishi wa umma huku akisisitiza wanasiasa wagombea kujiepusha na vitendo hivyo vinginevyo watalipia matendo yao hayo kwa uchungu mkubwa na kwa majonzi makubwa pale watakapofungwa jela.

Amewataka wananchi kutokubali kutumiwa na kikundi au mtu yeyote katika vitendo vya rushwa katika kuelekea kipindi hiki cha uchaguzi wa serikali za mitaa na kuwahimiza kutoka ushirikiano mkubwa.

Mkuu huyo wa Takukuru amesema katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia Aprili 2019 hadi June mwaka huu taasisi hiyo imefanikiwa kuwafikisha watuhumiwa 28 wa vitendo vya rushwa mahakamani huku watuhumiwa 18 wakiwa ni wajumbe wa mabaraza ya kata ya halmashauri ya wilaya ya Bukoba.

Amesema  taasisi hiyo itaendelea kuchukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na vitendo hivyo ambavyo vinafanywa na baadhi ya watu ambao kwa maksudi wanajaribu kujihusisha na rushwa na kwenda kinyume na sheria za nchi.

Amewataka watanzania kuhakikisha wanazuia na kupambana na rushwa kwamba taasisi hiyo inaendelea na mikakati mbalimbali ikiwemo kutoa elimu ya rushwa kwa umma.

Na Lydia Lugakila- Malunde1 blog Bukoba

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527