AMUUA MKEWE NA KUMTEKETEZA KWA MOTO WA MKAA GUNIA 2,KISHA KUZIKA MAJIVU YAKE

Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, linamshikilia mwanaume mmoja jina Khamis Luwonga maarufu kama 'Meshack' kwa tuhuma za kumuua na kumchoma moto mke wake Naomi Marijani (36).

Mwanamke huyo anadaiwa kutoweka katika mazingira ya kutatanisha na picha yake kusambazwa katika mitandao ya kijamii sanjari na taarifa za kutoweka kwake.

Mkuu wa Upelelezi kanda hiyo, Camillius Wambura amesema wanamshikilia mtuhumiwa kwa mahojiano na kwamba polisi wamekwenda kwenye maeneo ambayo mtuhumiwa aliyoyataja kufanyia mauaji na wamechukua majivu kwa ajili ya vipimo vya DNA ili kupata uthibitisho.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, inadaiwa kuwa Luwoga na mke wake Naomi hawakuwa na maelewano ya muda mrefu.

Kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kigamboni, Thobias Walelo mtuhumiwa huyo anayeshikiliwa na polisi kwa sasa, Khamis Luwongo (Meshack), amekiri kumuua mkewe na kisha kumchoma kwa mkaa magunia mawili na kumzika shambani kwake ambapo katika maelezo yake amedai mara baada ya mauaji hayo aliuchukua mwili wa mke wake na kuuweka kwenye shimo alilochimba kwenye banda lake la kufugia kuku.

Amedai baada ya kuuweka shimoni aliweka mkaa magunia mawili na mafuta ya taa kisha akawasha moto ulioteketeza mwili wote hadi kubaki majivu kisha alichukua majivu hayo akaweka kwenye mfuko na kubeba kwa kutumia gari lake lenye namba T206CEJ, Subaru Forester yenye rangi nyeusi na kuupeleka shambani kwake lililoko Kijiji cha Mlogolo, mkoani Pwani.

“Alichimba shimo kwenye shamba lake kisha kuweka hayo majivu, akayafukia na akapanda mgomba juu yake, kisha alikaa nyumbani kwake akisema mke wake ametoroka nyumbani Mei 15 na kufungua taarifa ya mke wake kutoroka nyumbani na kupewa RB ya kituo kidogo cha Mjimwema MJ/RB/234/2019.

Naomi alitoweka nyumbani kwake Mei 15, 2019, ambapo familia yake ilitoa taarifa za kutoweka kwake katika kituo cha Polisi Chang'ombe, baada ya Luwoga kuwapa taarifa siku nne baada ya Naomi kutoonekana nyumbani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527