JOGOO AFIKISHWA MAHAKAMANI KWA KUSUMBUA MAJIRANI ...'ANAWIKA SANA'


Jogoo huyu ambaye mmiliki wake amempatia jina la Maurice, amekuwa kero kwa majirani kwa kuwika kila alfajiri na malumbano kumhusu sasa yanajadiliwa katika mahakama moja nchini Ufaransa.

Analaumiwa kwa kusababisha kalele na familia moja katika kisiwa cha Oléron huko Ufaransa.

Mmiliki wake, Corinne Fesseau, anasema jogoo Maurice anafanya kile majogoo wote wanafanya 'kuwikaa'.

Waliomshtaki Maurice na Maurice mwenyewe hawakufika mbele ya mahakama ya mji wa magharibi wa Rochefort siku ya Alhamisi kesi ilipoanza kusikilizwa.

Lakini jogoo huyo ambaye amekuwa maarufu kutokana na kesi inayomkabili, amepata uungwaji mkono kutoka kwa wafugaji kuku wengine ambao walikusanyika nje ya mahakama.Corinne Fesseau akiwa na jogoo wake

Walalamishi, Jean-Louis Biron na Joëlle Andrieux, walijenga nyumba yao mapumziko katika kijiji cha Saint-Pierre-d'Oléron karibu miaka 15 iliyopita, lakini baadae wakaigeuza kuwa nyumba ya kuishi walipostaafu.

Sababu moja iliyowafanya kuchagua sehemu hiyo ni utulivu wake lakini tatizo ni kuwa jogoo Maurice, amekuwa kero kwao kwani amekuwa akiwapigia kelele kila aalfajiri anapowika.

Wanasema tatizo hilo lilianza tangu mwaka 2017 jirani yao alipomnunua.

Walipowasilisha lalama zao kwa Bi Fesseau, ambaye ameishi Oléron kwa miaka 35, mabishano makali yalizuka mpaka mzozo kati yao ukagonga vichwa vya habari ulipofikishwa mahakamani.

Bi Fesseau, na majirani zake wengine, walisema hakuna mjadala kuhusu swala hilo - kwa sababu ufugaji wa kuku ni sehemu ya maisha ya vijijini na kwamba hawaelewi kwa nini walalamishi wanaomba jogoo huyo azuiliwe kuwika.

Utatuzi wa mzozo huo unasalia na mahakama ambayo inasubiriwa kutoa uamuzi wa kesi mwezi Septemba mwaka huu.
Chanzo - BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527