WAZIRI MPINA AFUNGA KILELE CHA MAONESHO YA KWANZA YA NG’OMBE BORA WA MAZIWA TANZANIA , JIJINI DODOMA

Na.Fasustine Galafoni,Dodoma
Imeelezwa kuwa  idadi ya ng’ombe wa Kisasa waliopo Tanzania  kwa sasa ni zaidi ya Milioni Moja ambapo wana uwezo wa kuzalisha lita za Maziwa  zaidi ya Milioni 900  hivyo wafugaji wametakiwa kujikita katika ufugaji wa kisasa zaidi na wenye kuleta tija.

 
Akizungumza katika  Kilele cha maonyesho ya  kwanza  ya ng’ombe  bora  wa Maziwa tangu Tanzania ipate uhuru yaliyofanyika katika viwanja vya nanenane jijini Dodoma Juni 18,2019  ,Waziri wa  Mifugo na Uvuvi Mhe.Luhaga Mpina amesema ufugaji wa kisasa una tija kubwa katika maisha ya  Mfugaji kwani uhitaji mifugo wa chache huku wakitoa mazao mengi tofauti na ufugaji wa kienyeji ambapo umekuwa na mlundikano wa mifugo wengi na uzalishaji usiokuwa na tija katika kumwinua kiuchumi mfugaji.

Aidha,Waziri Mpina  amesema Zaidi ya Lita za Maziwa Milioni 20 kwa mwaka huagizwa kutoka nje ambapo hutumia zaidi ya Tsh.Bil.30 katika ununuzi huo hivyo kuna haja kubwa kwa Watanzania kujikita katika ufugaji wenye tija hali itakayosaidia upatikanaji wa maziwa kwa wingi hapa nchini kwani uzalishaji wa mbegu wan g’ombe wa Maziwa ni himilivu.

Waziri Mpina amesema kiwango mifugo 40  bora wa maziwa    ambayo imefanyiwa utafiti na Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI), na Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Mifugo International Livestock Research Institute (ILRI) bado ni michache hivyo kuna uhitaji mkubwa wa kuzalisha ng’ombe wa Maziwa.

Uzalishaji wa maziwa nchini kwa mwaka unakadiriwa kuwa lita bilioni 2.4. Wastani wa uzalishaji wa maziwa kwa ng’ombe bora mwenye damu mchanganyiko ni takribani lita 1,400 kwa msimu wa uzalishaji (lactation); wakati ambapo ng’ombe wa asili wanatoa wastani wa takribani lita 400 kwa msimu wa uzalishaji.

Hata hivyo,Waziri Mpina amesema Wizara yake ya Mifugo ina upungufu wa Watumishi ambapo kuna   kuna watumishi 3795 pekee katika halmashauri na amemwagiza katibu mkuu wa Wizara kufanya mchakato wa mgawanyo wa watumishi katika maeneo yaliyo na watumishi wachache huku pia akizitaka taasisi za kifedha kuchangamkia fursa ya kuwakopesha wafugaji  ili waweze kukuza tasnia yao ya ufugaji.

Naye Mkurugenzi Mtendaji wa  Taasisi ya Kimataifa ya Utafiti wa Mifugo International Livestock Research Institute (ILRI) Bw.Gimmy Symith amesema Kila nchi ambayo inafanya mchakato wa mabadiliko  kuwekeza katika viwanda vya kuzalisha maziwa  imeweza kubadilisha uchumi pia.

Programu ya Kuboresha Mbari za Ng’ombe Bora wa Maziwa (African Dairy Genetic Gains, ADGG) inafadhiliwa na Wakfu wa Bill & Melinda Gates, na ina nia ya kukuza ushirikiano kati ya wafugaji wa ng’ombe wa maziwa nchini Tanzania pamoja wadau ili kupambana na changamoto za ufugaji na kuongeza uzalishaji na
tija.

Maonyesho ya ng,ombe bora wa Maziwa yalianza tarehe 17  hadi 18 ,2019 ambapo ng,ombe 40  bora  hapa nchini wamebainika kuwa za uwezo wa kuzalisha zaidi ya  lita 30 kila mmoja kwa siku kwa mujibu wa tafiti za taasisi ya utafiti wa Mifugo Tanzania TALIRI Kwa kushirikiana na Taasisi ya utafiti ya Mifugo ya kimataifa ILRI ambapo kaulimbiu ni”ng’ombe bora kwa Maziwa zaidi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527