Wachimbaji Madini Lindi watoa kilio Tume ya Madini

Na Issa Mtuwa (Wizara ya Madini) Lindi na Mtwara
Mwenyekiti wa Tume ya Madini Prof. Idris Kikula amekutana na kilio cha wachimbaji wa madini mkoani Lindi kuhusu ongezeko la tozo zilizo kinyume cha sheria ya madini. Wakiongea kwa nyakati tofauti wachimbaji hao wamesema halmashauri za wilaya na vijiji zimekuwa zinawatoza tozo zaidi na ile iliyowekwa na sheria mama ambayo ni 0.03 badala yake wamekuwa wakitumia sheria ndogo (by law) zilizopitishwa na baraza la madiwani kuwatozo tozo zadi kinyume na sheria mama. 


Wameongeza kuwa halmashauri zinatoza tozo zao, na halmashauri za vijiji nazo zinajipangia ushuru wao kitu ambacho kina kuwa kero na kusababisha usumbufu kilio ambacho walikiwasilisha wakati wa mkutano mkuu wa sekta ya madini uliofanyika tarehe 22/01/2019 chini ya uenyekiti wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli. 


Prof. Kikula amekutana na kilio hicho akiwa ziara mkoani humo kutembelea na kukagua shuguli za madini, kusikiliza na kutatua kero za wadau wa madini. Kufuatia kilio hicho, Prof. Kikula ametoa wito kwa wachimbaji wa madini ya Gypsum, Kokoto, Chumvi na mchanga nchini kote kuwa na subira wakati Tume ya Madini ikihangaikia utatuzi wa changamoto hiyo ya utozwaji wa tozo zinazo tozwa na baadhi ya halmashauri za wilaya na vijiji kinyume na taratibu za sheria ya madini. 


Prof. Kikula ameyasema hayo leo mara baada ya kutembelea machimbo mbalimbali ya madini ya Gypsum ikiwemo ya kampuni ya KNAUF Gypsum Tanzania Ltd, machimbo ya Mavuji yanayomilikiwa na mchimbaji mdogo Faridu Sheweji na mchimbo ya chumvi yanayomilikiwa na Magereza Lindi eneo la  Machole.  


Akijibu hoja ya kero hiyo, mwenyekiti wa tume amekiri uwepo wa malalamiko ya namna hiyo kutoka kwa wachimbaji wa mikoa mbalimbali nchini na siyo kwa Lindi peke yake.  


Anashangazwa na hali hiyo kwa kuwa sheria ya madini na miongozo mbalimbali iko wazi na inaelekeza vizuri kuhusu tozo zinazotakiwa kutozwa. Amesema wao kama tume wanafanya jitihada kutatua kero hiyo, hivyo watawasilisha malalamiko yao kwa mamlaka ya juu ambayo ni Waziri mwenye dhamana ya madini Doto Biteko ili aweze kuzungumza na Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mita (TAMISEMI) Suleiman Jafo ili kuondoa kero hiyo.  


“Nalitambua hili tatizo, kila tunapofanya ziara mikoa mbalimbali hii changamoto inajitokeza, sijui ni kwa nini inakuwa hivyo kwa sababu sheria iko wazi namna tozo zinavyotakiwa kutozwa. Naomba niwaahidi tutalishugulikia hili haraka sana, na mara baada ya ziara hii tutaandaa ripoti na kuiwasilisha kwa Waziri Biteko, pamoja na ripoti lakini pia nitamwambia kwa mdodomo ili kusisitiza juu ya kero hii” amesema Prof. Kikula. 

Prof. Kikula ameziomba halmashauri na kila mdau wa madini kote nchini wazisome na kuzipitia vizuri sheria ya madini hususani inayohusu tozo mbalimbali za madini kabla ya kuanza kuwatoza wachimbaji. Mwenyekiti ameambatana na Kamishna wa Madini Prof. Abdulkarim Mruma walio anza ziara ya kikazi katika mikoa minne ya Lindi, Ruvuma, Njombe na Iringa katika kukagua shuguli za madini na kusikiliza na kutatua kero.  

Wakati huo huo mwenyekiti wa Tume ya Madini amefanya mazungumzo na wafanyakazi wa Tume hiyo wa mikoa ya Lindi na Mtwara kwenye ofisi za Afisa Madini Mkazi mkoa wa Mtwara. Amesikiliza kero za wafanyakazi hao hususani ukosefu wa watumishi na vitendea kazi. Kuhuusu magari amesema katika mwaka wa fedha ujao kila mkoa utapata gari jipya kuongezea yaliyopo na kuhusu watumishi suala hilo linafanyiwa kazi. Amewakumbusha kuhusu uadilifu katika kazi zao.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments