POLOKWANE FC WAZIDI KUIGANDA SIMBA SC


Kwa mujibu wa tetesi zilizopo, klabu ya Polokwane FC ya Afrika Kusini huenda ikamnasa mshambuliaji wa Simba, Adam Salamba baada ya kumkosa John Bocco. 

Dili hilo limekuja baada ya dili la mshambuliaji John Bocco kuingia dosari kwa kile kilichoelezwa kwamba Polokwane FC walimsainisha mchezaji huyo kimakosa, hivyo wameamua waikomalie Simba iwape mchezaji mmoja kwa mkopo.

Uongozi wa Simba kupitia Mtendaji Mkuu, Crescentius Magori umesema kuwa kumtoa Bocco ni ngumu kwa kipindi hiki hasa kutokana na malengo ya klabu ya Simba kwa sasa kuwa ya Kimataifa.

"Kumtoa mchezaji kama Bocco kwa sasa ni ngumu hasa ukizingatia Simba ni timu kubwa hivyo kumpeleka Afrika Kusini bado sio sahihi, hilo limeisha na viongozi wa Polokwane wameelewa na kwa sasa wanahitaji mchezaji wetu mmoja kwa mkopo", amesema Magori.

Adam Salamba amekuwa akitumia muda mwingi kwenye benchi la Simba, ambapo katika mchezo wa kirafiki wa Kimataifa kati ya Simba na Sevilla ya Hispania, Salamba alizua gumzo katika mitandao ya kijamii baada ya kuonekana akiomba viatu vya mshambuliaji wa Sevilla, Ever Banega.

CHANZO.EATV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527