MAKAMBA : TANZANIA TUNAO UWEZO MKUBWA WA KUZALISHA MIFUKO MBADALA


Na: Mwandishi Wetu
Tanzania inao uwezo mkubwa wa kuzalisha mifuko mbadala ambayo itatosheleza kufanikisha azma yake ya kupiga marufuku biashara na matumizi ya mifuko ya plastiki.


Hayo yamebainishwa na Waziri wa nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, mhe. Januari Makamba wakati akizungumza na Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa leo Jijini Dodoma. 


Makamba amesema kuwa ni jambo la kushangaza kuona asilimia 100 ya mifuko ya karatasi inayotumika nchini Rwanda na asilimia hamsini nchini Kenya inazalishwa Tanzania huku Tanzania ikitumia zaidi ya asilimia 80 ya mifuko ya plastiki inayozalishwa nje ya nchi jambo linalokinzana na dhana ya kukuza uchumi wa viwanda. 


“ Tunao uwezo mkubwa wa kuzalisha mifuko mbadala, wazalishaji wa mifuko hiyo wameithibitishia Serikali kuwa wanao uwezo mkubwa wa kuzalisha mifuko hiyo ambapo Kiwanda cha Karatasi cha Mufindi kimesema kitaongeza uzarishaji zaidi ya maratatu huku wawezkezaji zaidi ya 50 wakiwa wameagiza mashine za kuzalishia mifuko hiyo,”Alisema Waziri Makamba. 


Makamba aliongeza kuwa nchi ya Tanzania inaweza kufanikiwa katika zoezi hili kwa kuwa inazalisha mifuko mbadala ya karatasi ambayo hutumiwa kwa kiasi kikubwa na nchi jirani za  Rwanda huku kenya wakitumia asilimia kubwa ya mifuko kutoka Kiwanda cha Karatasi cha Mufindi cha hapa nchini, Kenya ikitumia asilimia 50, jambo linalotoa tafsiri kuwa tunaouwezo wa kuzalisha mifuko mbadala  itakayotosheleza,” Alisema Januari Makamba. 


Waziri Makamba amesema kuwa wazalishaji wa mifuko mbadala wameithibitishia Serikali kuwa wanao uwezo mkubwa wa kuzalisha mifuko hiyo ambapo Kiwanda cha Karatasi Mufindi kitaongeza uzalishaji zaidi ya mara tatu kinavyozalisha sasa huku wawekezaji zaidi ya 50 wakiwa wameagiza mashine kwa ajili ya kuzalishia mifuko hiyo. 


Katika hatua nyingine Waziri Makamba alitumia fursa hiyo kutoa rai kwa Wakuu wa Mikoa na Makatibu Tawala wa Mikoa kushirikiana kwa karibu na mamlaka zingine zitakazo husika katika zoezi la kutokomeza biashara na matumizi ya bidhaa za Plastiki zilizopigwa marufuku.

Akizungumzia marufuku hiyo Makamba amesema kuwa katika awamu ya kwanza marufuku hiyo inahusisha mifuko ya plastiki tu huku bidhaa zingine zinazotumia plastiki vifungashio vya plastiki kuendelea kutumika wakati utaratibu ukiendelea. Alizitaja bidhaa hizo kuwa ni bidhaa za chakula, kilimo na dawa. 


Utekelezaji wa katazo hilo la matumizi ya bidhaa za plastiki nchini linafuatia utekelezaji wa maelekezo ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli aliyotoa tarehe 26, April, 2019 katika maadhimisho ya Muungano jijini Dodoma. 


Mwisho.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527