RC MAKONDA KUWAKUTANISHA WADAU WA MICHEZO 1000 KUICHANGIA TAIFA STARS


Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam Mhe. Paul Makonda ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ushindi kwa timu za Taifa ameandaa hafla maalumu ya chakula cha jioni itakayoshirikisha wadau wa michezo wenye uzalendo na Timu yao ya taifa itakayofanyika  katika Hotel ya Serena na kushirikisha wadau zaidi ya 1,000.

Makonda amesema hafla hiyo itahusisha zaidi ya Kampuni 50 ambazo zimeomba kushiriki kama sehemu ya kuiwezesha Timu ya Taifa ambapo kila kampuni itatakiwa kuchangia kiasi cha shilingi Milioni 10 kwa meza moja zitakazotumika kuiwezesha Taifa Stars katika fainali za AFCON nchini Misri.

Aidha RC Makonda amesema hafla hiyo itarushwa Mubashara (LIVE) kupitia vyombo mbalimbali vya habari vilivyojitoa kuiwezesha Taifa stars huku akiwaomba wananchi kuendeleza uzalendo walioonyesha juzi.

Katika hatua nyingine RC Makonda kwa niaba ya kamati amewashukuru Wananchi,Wachezaji,wadau wa michezo,vyombo vya habari, watu mashuhuri na wamiliki wa Mahotel na Bar kwa umoja wa kitaifa walioonyesha katika mechi kati ya Taifa stars dhidi ya Uganda jambo lililowezesha Taifa Star kushinda na kufuzu AFCON.

Mhe. Makonda pia amewaomba wananchi na wadau kuonyeha uzalendo katika mashindono ya AFCON kwa vijana wenye umri chini ya Miaka 17 yanayotarajia kuanza April 14 jijini Dar es salaam Tanzania ikiwa mwenyeji wa mashindano hayo pamoja na kuishangilia Timu ya Wanawake ya Twiga Stars inayotaraji kucheza April 05.

Pamoja na hayo RC Makonda amemkabidhi kiasi cha Shilingi Milioni Moja kijana mzalendo kutoka Manyara aliesafiri kwa tabu kutoka Manyara hadi Dar es salaam akihamasisha wananchi kuwa wazalendo na Timu yao ya Taifa ambapo amewataka vijana wengine kuiga moyo huo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527