TFS YAFUNGA MTAMBO WA KUCHAKATA ASALI MANYONI

Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania(TFS) umefunga mtambo wa kuchakata asali wilayani Manyoni mkoani Singida.

Akizungumza jana Machi 14,2019 Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano TFS Tulizo Kilaga amesema mtambo huo wa kisasa una uwezo wa kuchakata lita 500 kwa siku.


Amesema kuwa mtambo huo umegharimu Sh.milioni 80 na unatarajiwa kuondoa changamoto ya uwepo wa asali yenye kiwango duni cha ubora katika ukanda huo na maeneo maeneo ya jirani.


“Mtambo huu umefungwa katika kiwanda cha TFS na utatumiwa na wafugaji wa nyuki wa ndani pamoja na nje wote wataruhusiwa kuchakata mazao yao,”amesema Kilaga.


Ameongeza kuwa kiwanda hiko kwa kiasi kikubwa kitategemea mali ghafi toka kwenye msitu wa Aghondi uliopo eneo la Itigi na uwepo


wa mtambo huo pia utasaidia kutunza mazingira kwani watakuwa na uhakika wa soko la asali yao.


Pia amesema katika uvunaji wa awali wamefanikiwa kuvuna mizinga 459 kati ya 729 na kupata asali kilo 6,175 sawa na tani 6.175 wastani kilo 13.45 kwa mzinga.


Akizungumzia mtambo huo, Meneja wa TFS wilayani Manyoni Juma Mambo amesema utasaidia kupatikana kwa asali bora na hivyo kuwa na uhakika wa soko la ndani na nje ambalo litawafanya wadau kujiongezea kipato.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527