Picha : TCRA YABAINI MADUDU YA KUTISHA KWENYE VITUO VYA REDIO..ITASHUSHA RUNGU ZITO MIEZI 4 WASIPOJIREKEBISHA


Mamlaka Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetoa miezi minne kwa Vituo vya Redio Kanda ya Ziwa kurekebisha mapungufu mbalimbali yaliyopo ikiwemo wafanyakazi kufanyishwa kazi bila mikataba ya ajira,vituo kukosa ubunifu wa kutafuta habari na matukio na kuwa watangazaji wa darasa la saba.

Akizungumza wakati wa Mkutano wa Watoa huduma za maudhui zikiwemo Redio,Tv na Mitandao ya Kijamii uliofanyika Machi 8,2019 jijini Mwanza, Mkuu wa TCRA Kanda ya Ziwa Injinia Francis Mihayo alisema vituo vya Redi vinatakiwa kufanya marekebisho vinginevyo vituo hivyo vitaamuriwa kusitisha huduma mpaka watakapojirekebisha.

Alisema hivi karibuni Kamati ya Maudhui ya TCRA ilifanya ukaguzi kwenye vituo vya Redio takribani 36 vilivyopo Kanda ya Ziwa  na kubaini kuwa vingi vina hali mbaya ya kiundeshaji na kiutendaji.

Aliyataja mapungufu yaliyopo kwenye vituo vya utangazaji vya Redio kuwa pamoja na wafanyakazi kutokuwa na mikataba ya ajira ambao baadhi ya vituo hakuna hata mmoja mwenye mkataba ajira lakini pia vituo vingine Watangazaji ni wa darasa la saba,Kidato cha Pili au Kidato cha Nne pamoja na kazi kutolewa kiukoo.

"Mapungufu mengine ni vituo kukosa vyoo na kama vipo basi ni vichafu lakini cha kushangaza kwenye ratiba yao ya vipindi wana vipindi vya afya,pia baadhi ya studio hazina Sound Proof,viyoyozi hali inayopelekea watangazaji kufungua madirisha pale wanapozidiwa na joto",

"Baadhi ya vituo vimekosa ubunifu wa kutafuta habari na matukio kunakopelekea ku kubadilisha ratiba ya vipindi bila kutoa taarifa TCRA,Mfano vipo vituo vya redio Wamiliki wake huamua kwa matakwa yao wenyewe kubadilisha vipindi kwa kuwaamrisha wakuu wa vipindi bila kufuata taratibu",alieleza.

Alisema mapungufu mengine ni baadhi ya vituo vya redio kutokuwa na mlinzi hata mmoja,vituo kutokuwa na mazingira rafiki ya kufanyia kazi, vituo kutolipia leseni kwa mujibu wa sheria na kushindwa kutoa taarifa za kweli pale TCRA inapoomba taarifa kutoka kwa watoa huduma.

Kutokana na mapungufu hayo,Mhandisi Mihayo alisema baada ya miezi minne iliyotolewa kujirekebisha wataamuru vituo vifungwe.

"Ni bora tuwe na vituo vichache vya redio vinavyofuata taratibu. Kuhusu mapungufu ya sifa (CV) za waajiriwa lipo kwa mujibu wa sheria ambapo serikali ilitoa muda mpaka ifikapo Desemba 2019 kila kituo lazima kiwe kina Wanahabari wenye kima cha chini cha elimu ya Diploma na si vinginevyo",aliongeza Mkuu huyo wa TCRA Kanda ya Ziwa.

Kwa upande wake,Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui TCRA, Bi Valerie Msoka alivitaka vyombo vya habari na waandishi wa habari kuzingatia maadili na sheria,kanuni za utangazaji na taratibu za nchi.

"Wasimamizi na Wamiliki wa vituo vya utangazaji lazima mtimize wajibu wenu ipasavyo,jitahidini kusimamia vipindi na ni vyema watangazaji wawe na Mwongozo wa Vipindi 'Script'",aliongeza.

Na Kadama Malunde - Malunde1 blog
Mkuu wa Mamlaka Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Ziwa Injinia Francis Mihayo akizungumza katika mkutano wa Watangazaji wa maudhui kutoka vituo vya Redio,Televisheni na Mitandao ya Kijamii Kanda ya Ziwa Machi 8,2019 katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Mwanza.

Mkuu wa Mamlaka Mawasiliano Tanzania (TCRA) Kanda ya Ziwa Injinia Francis Mihayo akizungumza katika mkutano wa Watangazaji wa maudhui kutoka vituo vya Redio,Televisheni na Mitandao ya Kijamii

Mwenyekiti wa Kamati ya Maudhui TCRA, Bi Valerie Msoka akizungumza katika mkutano wa Watangazaji wa maudhui kutoka vituo vya Redio,Televisheni na Mitandao ya Kijamii Kanda ya Ziwa Machi 8,2019 katika ukumbi wa ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Mwanza.

Wajumbe wa Kamati ya Maudhui TCRA wakiwa ukumbini.

Wajumbe wakiwa ukumbini


Mkurugenzi wa Malunde 1 blog, Kadama Malunde akiuliza swali wakati wa mkutano huo.
















Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527